BARAZA la NGO’s la Taifa, limeiomba Serikali kuzipa nafasi taasisi hizo zishauriane na wadau wake ili kutoa ushauri wa namna bora ya kutekeleza zoezi la kuhamisha wananchi kwa amani kutoka hifadhi ya Ngorongoro. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumatano tarehe 22, Juni, 2022 na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Lilian Badi, wakati akichangia mjadala katika mkutano wa mtandaoni, kuhusu uwekaji wa alama za mipaka tarafa ya Loliondo na maendeleo ya zoezi la uhamaji wa hiari kwa wakati wa Ngorongoro.
“Sisi kama baraza la NGO la Taifa tunaishukuru sana Serikali na tuko tayari kuishauri kwa mtazamo chanya tunaomba Serikali itupatie nafasi tushauriane na wadau wetu,” amesema Badi.
Amesema NGO’s zipo zaidi ya 7,000 nchini “na tutashauriana na wadau na kuweza kuleta mapendekezo kwa Serikali ili iweze kuitaarifu Serikali ni nini kinahitaji kufanyika katika kumaliza mchakato huo katika hali ya amani na utulivu.”
Amesema kama NGO’s wanaomba wananchi wasikilizwe “tunafahamu mabadilko na ubadiilishaji makazi ya watu si jambo rahisi kwahiyo sisi tupo tayari kuwaunga mkono katika kutoa uelewa tukiwa na utaalamu mkubwa wa kuelimisha wananchi kuhusu lengo la Serikali na nini kinaweza kufanyika katika suala zima la kuhamishwa kwenye makazi yao na kupelekwa maeneo ambayo Serikali imeyatenga kwa dhamira na maana nzuri zaidi.”
Amesema wanafahamu kuwa maendeleo lazima yatokane na watu wenyewe hivyo ni vyema watu hao waweze kusikilizwa.
Amesema baadhi ya NGO’s zimetoa taarifa kwa Baraza hilo kuwa zimeombwa zikutane na viongozi wa juu wa Serikali “tungeomba Serikali waweze kutoa nafasi hawa wadau waweze kusikilizwa ili kwa pamoja tuweze kutoa michango mizuri itakayosaidia zoezi la kuhamisha wananchi kwenda vizuri na kwa amani.”
Badi amesema pamoja na dhamira ya Serikali kuwa nzuri wamekuwa wakisikia taarifa za upotoshaji kwa Serikali na zoezi zima.
“Tumesikia kuna changamoto na tunajua kusimamia wananchi kuhama ni suala nyeti na linahitaji mikakati mingi na linahitaji kushirikisha sekta mbalimbali katika kuhakikisha linafanikiwa,” amesema Badi.
Leave a comment