TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nchini Tanzania imesema, kugongana kwa Tundu Lissu, Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Rais John Magufuli mkoani Kigoma, haiwezi kuathiri kampeni za Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Leo tarehe 19 Septemba 2020 Rais Magufuli alikuwa na shughuli ya kiserikali mkoani humo, ambapo amefanya mazungumzo na Rais wa Burundi, Evariste Ndayishimiye huku Lissu akiendelea na kampeni zake mkoani humo.
Dk. Wilson Mahela, Mkurugenzi wa Uchaguzi NEC amesema, hakuna tatizo lolote kwa kuwa Rais Magufuli ataendelea na shughuli zake wakati Lissu akiendelea na kampeni katika maeneo aliyopangiwa.
“Walioko Kigoma watajua namna ya kushughulikia, sababu yule mwingine si ataenda kwenye kampeni yake kama amepangiwa uwanja huu atafanya na nadhania Buhigwe anaenda jioni.”
“Sijaona changamoto sababu yule anaendelea na shughuli zake na yule anaendelea na kampeni zake,” amesema Dk. Mahera.
Kuhusu wagombea kubadili ratiba za kampeni, Dk. Mahela amesema ni jambo la kawaida kwa mgombea kuomba kubadili ratiba ya kampeni, ambapo NEC huwaruhusu kwa kuwa katika hali yakibinadamu ratiba haiwezi kwenda kama ilivyopangwa.
“Huwezi kusema kila kitu ukipange kiende kama kilivyo, sisi sio roboti ni binadamu, kuna mambo yatajitokeza katikati lazima yashughulikiwe na yeye kama Rais ikijitokeza ana mgeni wake lazima amhudumie,” amesema Dk. Mahela na kuongeza.

“Wagombea kubadili ratiba huwa ni changamoto lakini inapotoeka unatakiwa kukaa inaweza jitokeza ghafla mfano jana CUF alikuwa Tabora akataka kwenda Sikonge tukamruhusu akaenda na leo mgombea makamu wa rais wa Chadema Salum Mwalimu alikuwa hana nafasi ya kwena Sikonge akaomba abadilishiwe ratiba tumeruhusu hivyo huwa inajitokeza huwezi kukwamisha mambo.”
Jana Ijumaa tarehe 18 Septemba 2020 Lissu alifanya kampeni mkoani Katavi na leo anafanya kampeni katika maeneo ya Ikola Center, Buhigwe, Manyovu, Kigoma Kaskazini, Mwandiga na atamalizia Kigoma Mjini katika Uwanja wa Mwanga Center.
Kwa mujibu wa ratiba ya kampeni ya wagombea urais na makamu wa rais ya NEC, Rais Magufuli ambaye ni Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) alikuwa afanye kampeni Uvinza kisha mkoani Tabora.
Leave a comment