TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), hatimaye imeridhia takwa la mgombea ubunge wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (Chadema), katika jimbo la Singida Kaskazini, Djumbe David Djumbe. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mkurugenzi wa NEC, Ramadhan Kailima, amethibitishia MwanaHALISI Online, kuondolewa kwa mgombea huyo kwenye orodha ya wanachama wa vyama vya siasa waliopitishwa na tume yake kugombea nafasi hiyo.
“Unazungumzia Djumbe, huyo tayari ameondolewa kwenye orodha ya wagombea ubunge katika jimbo la Singida Kaskazini. Tumefanya hivyo, baada ya kutimiza masharti yanayotakiwa kwa mujibu wa sheria,” ameeleaza.
Djumbe alijitosa kwenye kinyang’anyiro hicho, kwa kile kilichoitwa na baadhi ya watu walioko karibu naye, “kupinga msimamo wa chama chake, kutoshiriki uchaguzi huo.”
Hatua hiyo ya Djumbe, ilizua tafrani kubwa ndani ya chama hicho. Viongozi kadhaa wa chama hicho, walimtafuta kwa njia mbalimbali kumuomba ajiondoe kwenye kinyang’anyiro hicho.
Mkanganyiko ndani ya Chadema ndiyo uliosababisha jina la Djumbe kupelekwa NEC na kupitishwa kuwa mgombea ubunge Singida Kaskazini.
Wakati Chadema ngazi ya Taifa ikisema haitashiriki katika uchaguzi huo hadi NEC itakapokutana na wadau kujadili changamoto zilizojitokeza katika uchaguzi wa udiwani katika kata 43, uongozi wa chama hicho mkoani Singida ulipeleka Tume jina la Djumbe kuwa mgombea.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Singida, Shaban Limu amesema Djumbe aliteuliwa kugombea na kamati ya utendaji ya wilaya.
Amesema wakati anateuliwa uongozi wilaya na mkoa ulikuwa haujawasiliana na Makao Makuu kujua msimamo juu ya uchaguzi huo.
Mkanganyiko ndani ya Chadema ndiyo uliosababisha jina la Djumbe kupelekwa NEC na kupitishwa kuwa mgombea wa ubunge katika jimbo hilo.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya chama hicho, marufuku ya makao makuu ya kususia uchaguzi hadi NEC itakapokutana na wadau kujadili matatizo yaliyojitokeza kwenye uchaguzi wa udiwani katika kata 43, Chadema mkoani Singida, kwa kauli moja, kilimpitisha Djumbe kuwa mgombea wake.
Mwenyekiti wa Chadema mkoani Singida, Shaban Limu amesema, Djumbe aliteuliwa kugombea na kamati ya tendaji ya wilaya yake na hivyo anazo sifa zote za kuwa mgombea.
Katika maelezo yake kwa MwanaHALISI Online Kailima anasema, “baada ya kutimiza masharti hayo, NEC imemuondoa kwenye orodha ya wagombea. Hii ni kwa sababu, suala la kujitoa kwenye kinyang’anyiro, ni jambo la hiyari.”
Tarehe 20 Desemba, Djumbe aliwasilisha nyaraka za kujitoa katika uchaguzi huo uliopangwa kufanyika 13 Januari mwakani.
Kifungu cha 49 (1) (2) cha sheria ya uchaguzi, sura 343 kinaeleza kuwa mgombea anaweza kujitoa kwa kuandika barua na kuisaini yeye mwenyewe pamoja na ahadi ya kiapo cha sheria alichoapa mbele ya hakimu. Djumbe amekidhi hitaji hilo la kisheria.
Jimbo la Singida Kaskazini liko wazi baada ya aliyekuwa mbunge kwa tiketi ya CCM, Lazaro Nyalandu kujivua uanachama wa chama hicho na kujiunga Chadema hivyo kupoteza nyadhifa zake zote za chama na ubunge.
Uchaguzi huo wa marudio utafanyika pia katika majimbo mengine mawili ya Longido na Songea Mjini.
Uchaguzi katika jimbo la Longido unafanyika kufuatia matokeo ya uchaguzi wa ubunge ya mwaka 2015 kubatilishwa na mahakama.
Nako jimboni Songea Mjini, uchaguzi unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wake, Leonidas Gama (CCM), kufariki dunia.
Leave a comment