TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) inaanza kutoa fomu za uteuzi kwa wagombea urais wa Tanzania na makamu wake, kuanzia leo Jumatano tarehe 5 -25 Agosti 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya NEC imeeleza, fomu hizo zitatolewa ofisi za tume hiyo Njedengwa jijini Dodoma.
Uteuzi wa nafasi hizo itakuwa tarehe 25 Agosti 2020 ofisi za NEC, Dodoma.
Pia, fomu za uteuzi kwa wagombea ubunge, zitatolewa tarehe 12-25 Agosti 2020 katika ofisi za halmashauri nchini.
Fomu za udiwani zitatolewa tarehe 12-25 Agosti 2020 katika ofisi za kata husika.
Kampeni zitafanyika kuanzia tarehe 26 Agosti 2020 hadi 27 Oktoba 2020 na uchaguzi mkuu utafanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
Tayari vyaka mbalimbali vya siasa nchini vimepitisha wagombea urais ndani ya vyama vyao ili kushiriki uchaguzi huo.
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimempitisha Rais John Pombe Magufuli na mgombea wake mwenza ni, Samia Suluhu Hassan.
Tundu Lissu, amepitishwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) huku Salum Mwalimu akipitishwa kama mgombea mwenza.
Wengine ni; John Shibuda wa Ade-Tadea, Profesa Ibrahim Lipumba wa Chama Cha Wananchi (CUF) na Hashim Rungwe wa Chaumma.
Leave a comment