NDUGU wa Tarimo Nemes Raymond Raia wa Tanzania aliyefariki kwenye uwanja wa vita katika mji wa Bakhmut nchini Ukraine akipigana upande wa Urusi dhidi ya Ukraine wamedai hadi sasa wametumia siku 10 kuusubiri mwili wa ndugu yao kwa kulala matanga. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa zinaeleza kuwa kifo cha Nemes aliyekuwa anaipigani Uruso kupitia kikosi cha mamluki cha Wagner kinachomilikiwa na Yevgeny Prigozhin swahiba wa Rais wa Urusi, Vladimir Putin, kimetokea tangu Oktoba 2022 lakini habari za kifo hicho zimefahamika jana baada ya kuripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari.
Akizungumza na MwanaHalisi Online leo tarehe 18 Januari, 2023 jijini Dar es Salaam, Mjomba wa Nemes, Andrew Mwandenuka amesema familia hiyo ilipewa ahadi ya kuwa mwili huo utafika nchini hivi karibuni na kupata matumaini baada ya kuona picha mwili huo ukiagwa huku Urusi.
“Tupo hapa tunasubiri mwili wa Nemes kila siku tunaambiwa utakuja lakini juzi tumeona anaagwa pengine wanamaliza taratibu utaletwa na hivi karibuni tumeambiwa huenda ijumaa ya wiki hii utaletwa sisi tunaendelea kusubiri” amesema Mwandenuka.
Amesema msiba huo kwa upande wao una gharama kutokana watu kujianda kwa msiba kwa matumaini ya kuwa wataupata mwili wa ndugu yao bila mafanikio kwa siku 10 sasa.
Kwa upande wa Dada wa Nemes , Salome Kisale ameishukuru Serikali kwa kuwapa ushirikiano na kupata taarifa ya kifo cha ndugu yao.
“Tunamshukru Rais Samia pamoja na watendaji wake nchini Urusi kwa kweli wanatupa ushirikiano na tuna matumaini kuwa watatusaidia kuupata mwili wa ndugu yetu”.
Salome alipoulizwa kama anajua taarifa za ndugu yao kufariki vitani alikanusha akajibu kuwa Nemes hajafia vitani.
MwanaHALISI Online itaendelea kukujuza kinachoendelea kuhusu kifo cha Nemes.
Leave a comment