SPIKA wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai, anatarajiwa kufika mjini Nairobi leo au kesho Alhamisi kumtembelea mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu. Anaripoti Mwandishi Wetu kutoka Nairobi….(endelea).
Taarifa kutoka Bunge la Tanzania na familia ya Lissu jijini Dar es Salaam na mkoani Singida zinathibitisha kuwa Ndugai atakwenda Nairobi kumjulia hali Lissu na kupata taarifa ya matibabu yake.
“Ni kweli kuwa Spika Ndugai atakwenda Nairobi kati ya leo (Jumatano) na kesho Alhamisi kumuona mheshimiwa Lissu. Mipango ya safari hiyo inaratibiwa na familia ya Lissu na baadhi ya marafiki zake wa karibu,” ameeleza mmoja wa wanafamilia wa mbunge huyo.
Amesema, “Ndugai anakwenda Nairobi kuonana na Lissu, kwa lengo la kuzunguza naye juu ya matibabu yake. Anakwenda kwa lengo la kujua maendeleo ya afya ya mbunge huyo na jinsi alivyoathirika na majeraha ya risasi.”
Kupatikana kwa taarifa hizi kumekuja kipindi ambacho, Lissu amekuwa akinukuliliwa kulalamikia Ndugai kuwa “amemtekeleza” Nairobi.
Spika huyo wa Bunge, hajakwenda Nairobi kumuona mbunge wake, tangu mwanasiasa huyo kupelekwa mjini humo Septemba mwaka huu.
Lissu alishambuliwa kwa risasi za moto na wanaoitwa na serikali, “watu wasiofahamika,” nyumbani kwake, majira ya saa saba na nusu mchana akiwa ndani ya gari eneo la Area D, mjini Dodoma.
Kabla ya kupelekwa Nairobi, Lissu alitibiwa katika hospitali ya mkoa wa Dodoma.
Taarifa kutoka familia ya mwanasiasa huyo na Lissu mwenyewe zinasema, mbunge huyo wa Singida Mashariki, anatarajiwa kuondoka mjini Nairobi, Jumamosi wiki hii.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Lissu anapelekwa moja ya nchi za Ulaya, jina na hospitali anayokwenda tunaihifadhi kwa sasa.
Leave a comment