Job Yustino Ndugai, Spika wa Bunge, amejiapiza kutoruhusu wabunge wanaotumikia adhabu mbalimbali kurejea Bungeni hata kama wataenda kupinga suala hilo katika mamlaka zingine zozote, anaandika Dany Tibason.
Amesema ni lazima wabunge waliofukuzwa watumikie adhabu za kusimamishwa kwa muda wa mwaka mmoja na kwamba hawatarudi Bungeni kabla ya kumaliza adhabu hiyo.
“Wenzetu ambao muda mwingi wanakuwa hawapo, wakija wanachafua hali ya hewa na kisha wanaondoka, anasimama mtu hapa bungeni na kusema Bunge hili ni dhaifu, kwasababu hiyo unawaona wenzako waliochaguliwa ni dhaifu.
“Wakati mwingine utawala unauharibu na kuutengeneza wewe mwenyewe, unasema utawala dhaifu si unamfanya mtawala aamue kugangamala?
“Aliyefanya agangamale ni nani kama sio wewe na mdomo wako? mara mnakimbia huku na kule, hakuna kesi wala nini, nasema mimi ndio Spika, mwaka mzima hakanyagi mtu hapa ndani hata mkienda wapi,” amesema Ndugai.
Itakumbukwa kuwa, Wabunge Halima Mdee (Kawe), Ester Bulaya (Bunda Mjini) na John Mnyika (Kibamba) wamefungua kesi katika Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma wakipinga kufungiwa kushiriki vikao vya Bunge bila ya kupewa nafasi ya kujitetea.
Mdee na Bulaya wamezuiwa kuhudhuria vikao vya Bunge kwa muda wa mwaka mmoja huku Mnyika akifungiwa vikao vitano – hata hivyo tayari adhabu yake imemalizika na amerjra Bungeni.
Aidha, Ndugai amesema amepokea miswada mitatu kwa hati ya dharura kutokana na mambo nyeti yaliyopo ndani ya miswada hiyo na kwamba kuna umuhimu wa kuijadili na kuipitisha kwa wakati huu.
“Pamoja na mambo mengine, inalenga kuboresha ushiriki na umiliki wa watanzania katika masuala ya madini. Madini yasiyochenjuliwa hayatasafirishwa tena nje ya nchi, na hili nalo nilirudishie huko huko?
“Linakuja jambo la kupunguza mamlaka ya waziri na Kamishna wa Madini, mlikuwa mnapiga kelele kwenye hili, nalo nilikatae lisije Bungeni?” amehoji Ndugai.
Leave a comment