HATUA ya Job Ndugai, Spika wa Bunge kumwingiza Rais John Magufuli kwenye mgogoro wake na Prof. Mussa Assad, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), imekosolewa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Ushirika wa vyama vinane vya upinzani nchini, umemtaka Spika Ndugai kuacha kuhusisha mgogoro wake na Ofisi ya Rais na kwamba, kufanya hivyo ni kuingiza taasisi nyingine isiyohusika.
Jana tarehe 14 Aprili 2019, akizungumza na waandishi wa habari Spika Ndugai alisema kwamba, Prof. Assad aende kwa Rais Magufuli kukiri kosa kwa kauli yake kwamba, Bunge ni dhaifu.
“ . ..aende kwa rais, amueleze rais kwamba, aliteleza ..matusi hayo anayoyatoa kwa Bunge anamtukana kila mtu, rais yupo mule,Waziri mkuu yumo mule, Baraza la mawaziri wapo mule anautukana hadi mkono unaomlisha,” alisema Spika Ndugai.
Hata hivvyo, muungano huo unaoundwa na Chadema, ACT-Wazalendo, CHAUMMA, DP, CCK, UPDP, NLD na NCCR – Mageuzi umemtaka Spika Ndugai ‘kuchonganisha’ ofisi hizo mbili (Ofisi ya Rais na Ofisi ya Bunge’ kwa kuwa, zenyewe hazina mgogoro.
Fahmi Dovutwa, Mwenyekiti wa UPDP amesema kuwa, hatua ya Spika Ndugai kuuingiza mgogoro wake na CAG katika Ofisi ya Rais ni kuukuza.
“Spika anataka nini kwa rais, yeye aende kwenye maslahi ya umma,” amesema Dovutwa na kuongeza; “jambo hili linahitaji umakini.”
Hata hivyo, wakati Spika Ndugai akimshauri Prof. Assad kujiuzulu, kibao hiko kimemgeukia mwenyewe kwamba, ameshindwa kuongoza Bunge hivyo ajiuzulu.
Ushirika huo umetolewa kauli hiyo leo tarehe 15 Aprili 2019, mbele ya waandishi wa habari katika Ofisi ya Chadema, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Ushirika huo umemtuhumu Spika Ndugai kwamba, anaongoza Bunge kwa utashi wake huku akipuuza matakwa ya umma.
Dovutwa amesema kuwa, kwa hatua Bunge lilipofikishwa sasa, hakuna budi Spika Ndugai kung’oka.
“Kwa hapa lilipofikishwa Bunge, maoni ya wananchi yasikilizwe. Bunge lipokee hoja za wananchi na zizingatiwe. Leo amemkata CAG kesho akiwa na kesi mahakamani atamkataa Jaji Mkuu,” amesema Dovutwa.
Leave a comment