MABIGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Simba imetangaza kuachana na kocha wake mkuu, Sven Vandenbroeck. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
Simba imetangaza kuachana na Sven Alhamisi usiku tarehe 7 Januari 2021 kupitia taarifa kwa umma iliyotolewa na timu hiyo, ambayo haikueleza sababu ya uamuzi huo.
Sven ameachana na Simba baada ya kuifikisha hatua ya makundi ya Klabu Bingwa Afrika kwa kuitoa FC Platinum ya Zimbambwe kwa magoli 4-0 kwenye mchezo wa marudiano uliochezwa Uwanja wa Benjamim Mkapa Dar es Salam.
Katika mchezo wa kwanza uliochezwa wiki mbili zilizopita, Harare nchini Zimbabwe, Simba ilifungwa goli 1-0.
Sven ameondoka Simba akiwa ameichia mafanikio msimu uliopita kwa kutetea kombe la ligi kuu, kutwaa kombe la shirikisho na ngao ya jamii.
Taarifa hiyo ya Simba imesema, kocha msaidizi, Suleiman Matola ataiongoza timu hiyo hadi atakapopatikana kocha mwingine.
Simba kwa sasa iko visiwani Zanzibar kushiriki michuano ya mapinduzi ambapo leo Ijumaa saa 10:15 jioni itashika dimbani kucheza na Chipukizi.
Leave a comment