CHAMA cha siasa cha upinzani nchini Tanzania cha NCCR-Mageuzi kimeanza kugawa vifaa vya uchaguzi kama bendera, katiba na kadi kwa wagombea wake wa ubunge katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea)
Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo Jumamosi tarehe 1 Agosti 2020 na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa NCCR- Mageuzi, Anthony Komu kwa wagombea ubunge wa Bahi, Melkzedek Lesaka na Fataha Amir Ibrahim wa Chemba wa Mkoa wa Dodoma.
Wagombea wengine watakaonufaika na vifaa hivyo katika Mkoa wa Dodoma ni wa Dodoma Mjini, Kondoa Mjini, Kondoa Vijjijini na Chamwino zamani liliitwa Chinolwa.
Mara baada ya kukabidhi vifaa hivyo, Komu amewataka wagombea hao wawili, kutumia rasimali hizo za chama kwa ujenzi wa chama na kuhakikisha wanashinda uchaguzi huo kwa kishindo.
Naye Fatah amesema, atavitumia vifaa alivyokabidhiwa kuendesha chama na kwamba ana matarajio makubwa watashinda uchaguzi huo.
Fatah amesema, NCCR- Mageuzi, tayari imeweka wagombea sita kati ya majimbo tisa yaliyopo katika mkoa huo na katika jimbo la Dodoma Mjini, wameshasimisha madiwani 30 katika kata 41 zilizopo.
Katika uchaguzi mkuu uliyopita, Fatah aligombea ubunge katika jimbo hilo la Chemba kupitia ACT Wazalendo, ambapo alishika nafasi ya pili, nyuma ya Juma Nkamia.
Katika kura za maoni za Chama Cha Mapinduzi (CCM), zilizomalizika hivi karibuni, Nkami alishindwa kutetea kiti chake baada ya kushika nafasi ya pili.
Leave a comment