BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) tawi la Mwanza imetoa msaada wa mifuko ya saruji 200 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa katika shule ya Msingi Samia iliyoko wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza sambamba na msaada wa madawati 50 kwa ajili ya shule za msingi zilizopo wilayani Ilemela mkoani humo ikiwa ni hatua ya benki hiyo kuunga mkono juhudi za serikali pamoja na wananchi katika kuboresha elimu wilayani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza kwenye hafla za kukabidhi misaada hiyo leo tarehe 12 Oktoba, 2022, Meneja wa benki ya NBC Tawi la Mwanza, Thomas Lijaj alisema misaada hiyo inalenga kuunga mkono jitihada ambazo tayari zinaendelea kuonyeshwa na serikali pamoja na wananchi katika maeneo husika kwa kuboresha miundombinu ya elimu.
“Tunaamini kwamba mifuko ya saruji pamoja na madawati tuliyoikabidhi katika halmashauri hizi mbili zitasaidia kuunga mkono jitihada ambazo tayari zipo katika kutatua changamoto zilizopo za uhaba wa vyumba vya madarasa na madawati katika shule husika. Lengo ni kuwasaidia wanafunzi wapate mazingira bora zaidi ya kujifunzia,’’ alisema Lijaj.
Aliipongeza serikali kwa jitihada inazoendelea kuzionesha katika kuboresha elimu hapa nchini huku akibainisha kuwa benki ya NBC kama mdau muhimu wa maendeleo itandelea kuunga mkono jitiha hizo huku lengo likiwa ni kuongeza kasi ya maendeleo katika sekta hiyo muhimu.
“Lengo letu ni kuhakikisha ndoto za watoto hawa kielimu zinafikiwa na pia kumuunga mkono Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassani katika utoaji wa elimu bora. Kwa hiyo tumekabidhi madawati na mifuko ya saruji kwa ajili ya wanafunzi hawa kwa kuwa ni furaha ya NBC kuona watoto wanaondokana na changamoto mbalimbali zinazowakabili hasa katika swala la elimu” aliongeza Lijaj.
Wakizungumza mara baada ya kupokea misaada hiyo Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Bi Amina Makilagi na Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Bw Hassan Masala pamoja na kuishukuru benki hiyo kwa msaada huo walisema serikali imejipanga kuhakikisha inamaliza changamoto za kielimu kupitia mipango yake mbalimbali sambamba na kushirikiana na wadau mbalimbali zikiwemo taasisi za kifedha.
“Msaada huu umekuja wakati muafaka kwasababu tunahitaji madawati kwa ajili ya wanafunzi watakaonza masomo mapema mwakani…tunawashukuru sana benki ya NBC kwa kutuunga mkono kwenye hili,’’ alisema Masala.
Kwa upande mmoja wa wakuu wa shule hizo, Mbita Samson ambae ni Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Samia aliishukuru benki ya NBC kwa namna ilivyoguswa katika kuchangia sekta ya elimu ikiwemo ujenzi wa vyumba vya madarasa na msaada wa madawati kwa kuwa jitihada hizo zimekuwa zikisaidia kuongeza kasi ya serikali na wanachi wanaojitolea kuboresha utoaji wa elimu hapa nchini.
“Binfasi nimefarijika sana kwa msaada huu kutoka NBC na kwa kweli bado tunahitaji wadau wengine wajitoe kusaidia kama walivyofanya benki hii. Hii leo tumepokea msaada huu mifuko ya saruji itakayotusaidia sana kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa hivyo tunawashukuru sana kwa kuunga mkono jitihada za wananchi na serikali yetu…asanteni sana NBC,’’ alisema Mbita
Leave a comment