MKUU wa Wilaya ya Mtwara, Dastan Kyobya ameiomba Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kuangalia uwezekano wa kuongeza zaidi matawi yake katika mikoa ya Mtwara na Lindi ili kuwafikia zaidi wakulima wa korosho wa mikoa hiyo ambao kwasasa wanahitaji huduma rafiki za kibenki huku wakionesha kuvutiwa zaidi na huduma ya akaunti ya NBC Shambani inayotolewa na benki hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza mwishoni mwa wiki mkoani humo wakati wa hafla fupi ya kukabidhi ya zawadi mbambali kwa wakulima wa korosho mkoa wa Mtwara walioibuka washindi wa droo ya pili ya kampeni ya ‘Vuna Zaidi na NBC Shambani’, Kyobya alisema pamoja na kuhitaji huduma za kibenki zilizo karibu zaidi na maeneo yao wakulima wa korosho katika mikoa hiyo wanahitaji huduma zinazoendana na mahitaji ya kilicho cha zao husika.
“Muitikio huu mkubwa unaoshuhudiwa sasa kwa wakulima wa korosho kujiunga zaidi na benki ya NBC ni ushahidi tosha kwamba wakulima wanauhitaji zaidi na huduma zinazoendana na mahitaji yao. Jitihada hizi za NBC zimeonesha kuunga mkono juhudi za wakulima na serikali katika kuboresha kilimo cha korosho katika mikoa ya Mtwara na Lindi‘’
“Zaidi pia zawadi zinazotolewa kupitia kampeni hii ikiwemo baiskeli, pikipiki, pampu za kupulizia dawa mikorosho, guta (Toyo) pamoja na zawadi za nyingine ikiwemo kanga, mabegi ya shule na madaftari ni ushuhuda tosha kwamba huduma hii kweli inalenga kuchochea kilimo cha zao la korosho vinginevyo mngeweza kuwapatia wakulima zawadi nyingine ambazo haziendani na mahitaji ya kilimo cha zao la korosho…hongereni sana,’’ alisema.
Alisema kupitia muitikio huo ipo haja ya benki hiyo kuongeza matawi yake ikiwemo huduma ya uwakala wa kibenki katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo ili wakulima hao waweze kunufaika zaidi na huduma hizo zinazoambatana na mikopo ya zana za kilimo na ushauri wa kitaalamu kuhusu kilimo cha kisasa.
Zaidi, aliwataka wakulima hao kutumia vifaa hivyo ipasavyo ili viweze kuwasaidia katika kuhakikisha wanaongeza uzalishaji wa zao hili kwa kujiandaa vema kwa ajili ya msimu ujao.
Kwa upande wake Meneja wa Benki hiyo Kanda ya Kusini Bi Zubeider Haroun alisema kupitia droo hiyo ya pili benki ilitoa zawadi za aina mbalimbali zipatazo 23 ikiwemo pikipiki 3, baiskeli 10, pampu za kupulizia dawa mikorosho 9, guta (Toyo)1, pamoja na zawadi za nyingine ikiwemo kanga, mabegi ya shule na madaftari kwa wakulima mmoja mmoja na AMCOS katika mikoa ya Mtwara na Lindi.
“Kampeni hii inalenga kusaidia jitihada zilizowekwa na serikali za kuongeza uzalishaji wa korosho kutoka tani 280,000 zinazozalishwa sasa hadi kufikia tani 700,000 ifikapo mwaka 2025 sambamba na kuwahamasisha wakulima wa korosho kufanya kazi kwa bidii ili kuongeza uzalishaji.’’
“Naendelea kuwahamasisha wakulima waendelee kupitishia fedha zao kupitia benki akaunti ya NBC Shambani ili wawe kwenye nafasi kujishindia zawadi lukuki katika droo zinazofuata,’’ alisema Bi Zubeider
Kwa upande wao washindi wa droo hiyo waliishukuru benki ya NBC kwa kuandaa kwa kampeni hiyo kwa kuwa imekuwa na msaada mkubwa kwao.
“Mbali na zawadi mbalimbali ambazo tumefanikiwa kupata kupitia kampeni hii ya Vuna Zaidi na NBC Shambani’’ tunashukuru pia tumepata hamasa na elimu ya kutosha kuhusu kilimo cha zao hili kibiashara zaidi.’’ Alisema Bw Shabani Mangoni Mwenyekiti AMCOS ya Kilomba iliyopo Mkoani Mtwara.
Leave a comment