BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) leo tarehe 4 Oktoba 2021, imezindua wiki ya Huduma kwa Wateja sambamba na kampeni maalum inayofahamika kama ‘Nguvu ya Huduma, Zege Halilali’ ambayo ni kielelezo na chachu ya utoaji wa huduma kwa haraka na kwa wakati kulingana na mahitaji ya wateja wa benki hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Uzinduzi wa kampeni hiyo ya mwezi mmoja umeanza leo na kushuhudiwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Theobald Sabi kwa kushirikiana na viongozi waandamizi wa mamlaka mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) walizindua huduma ya uwakala wa malipo ya kodi na tozo mbalimbali za mamlaka hizo itakayotolewa na benki hiyo hadi usiku.
“Utoaji wa huduma kwa wateja kwa kuzingatia weledi na kwa wakati ndio msingi wa mafanikio kwetu kama benki na kwa wateja wetu. Lengo hasa la kampeni ya ‘Nguvu ya Huduma, Zege Halilali’ ni kuakisi mkakati huo tukizingatia kwamba wateja wetu wengi hususani wafanyabiashara hawana muda wa kupoteza. Hivyo sisi kama benki lazima twende na kasi hiyo na ndio sababu kupitia huduma hii wataweza kufanya malipo yao ya TRA na Bandari hadi usiku kupitia benki ya NBC,’’ alifafanua Sabi.
Amesema katika kufanikisha dhana hiyo ya ‘Nguvu ya Huduma, Zege Halilali’ benki hiyo imeendelea kuwekeza zaidi katika huduma za kidigitali ili kutoa huduma zake kwa haraka na wakati sambamba na kuongeza idadi ya matawi pamoja na mawakala wa benki hiyo kila maeneo mengi hapa nchini.
“Kasi hii ya utoaji huduma inakwenda sambamba na ongezeko la huduma zetu mbalimbali zinazobuniwa kwa kuzingatia mahitaji ya wateja wetu ikiwemo huduma ya NBC Shambani mahususi kwa wakulima pamoja na ‘NBC Kua Nasi’ mahususi kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo.’’ amesema.
Akizungumzia ujio wa huduma ya uwakala wa malipo ya kodi na tozo kupitia benki ya NBC, Naibu Kamishna Forodha na Ushuru wa TRA Bw Godfrey Kitundu alisema huduma hiyo imekuja wakati sahihi na kwa kiasi kikubwa itawasaidia wafanyabiashara wanaotumia bandari ya Dar es Salaam pindi wanapohitaji kufanya malipo ya kodi na tozo za TRA na Mamlaka ya Bandari hata nyakati za usiku.
“Kimsingi ni kwamba ‘Nguvu ya Huduma, Zege Halilali’ imekuja wakati sahihi kwa kuwa ni wazi kwamba kwasasa wafanyabiashara ambao walikuwa wakilazimika kusubiri siku inayofuata ili tu kufanya malipo ya kodi na tozo za TRA na Bandari. Kupitia huduma hii sasa wataweza kufanya malipo hayo hata usiku kupitia benki ya NBC.’’
“Hatua hii inaungwa mkono na sisi kama Mamlaka ya Mapato pamoja na serikali kwa ujumla kwa kuwa itatochochea ukusanyaji wa mapato na ukuaji wa uchumi…tunawapongeza sana NBC kwa hili,’’ amesema.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo Meneja wa Huduma kwa Wateja wa benki hiyo, Salama Musa amesema benki hiyo imejipanga kuutumia maadhimisho hayo kama fursa nzuri ya kuboresha zaidi muonekano wake kwa mamia na maelfu ya wateja wake kote nchini.
“Tumetenga mwezi mzima kwa ajili ya huduma maalum kwa wateja wetu kwa kutambua na kuthamini nafasi yao muhimu katika kuifanya Benki ya NBC kuwa benki kubwa na yenye faida zaidi nchini. Hii inakuja wakati ambapo pia tumewekeza zaidi katika kuwasogezea huduma zetu mahali popote walipo kupitia matawi, mawakala na huduma zetu za kidigitali,’’ amesema.
Wakizungumzia huduma za benki hiyo baadhi ya wateja walisema wameguswa na benki hiyo sio tu katika kuhifadhi pesa zao au maswala ya mkopo bali pia benki hiyo imekuwa mstari wa mbele katika kuwasaidia kutatua changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo katika shughuli zao za kila siku.
“Kimsingi ni kwamba ninafurahia sana huduma za Benki ya NBC. Imekuwa ni kwa kipindi cha muda mrefu nimekuwa nikishirikiana na benki hii na kiukweli ninaridhishwa zaidi na utamaduni wao wa kazi na maadili ya taaluma yanayotoa fursa kwangu kuendelea kufanya kazi pamoja katika kufanikisha shughuli zangu..’’ amesema Anita Waitara, mmoja wa wateja wa benki hiyo.
Kivutio katika hafla hiyo ilikuwa ni kitendo cha wafanyakazi pamoja na watendaji wakuu wa benki hiyo wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo Bw Theobald Sabi waliowakaribisha kwa kuwapigia makofi ya heshima wateja wa benki hiyo waliokwenda kupata huduma kwenye tawi la Samora jijini Dar es Salaam huku wateja hao pia wakionesha kufurahishwa na kuipokea heshima hiyo.
Leave a comment