JEAN Marc Ayrault Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa amesema Jumuiya ya Umoja wa Nchi za Kujihami za Ulaya (NATO), zishirikiane kumjibu Donald Trump Rais mteule wa Marekani anayeeneza propaganda za kusambaratika kwa jumuiya hiyo, anaandika WolframMwalongo.
Ayrault amependekeza njia hiyo itumiwe kumfunga mdomo Trump ambaye amekuwa akidai baadhi ya nchi wanachama wa NATO zimekuwa zikisota kutoa michango na kwamba kwa sasa baadhi ya nchi zipo kwenye harakati za kujitoa kwasababu jumuiya hiyo imepitwa na wakati.
Huu ni muendelezo wa Trump kuzishambulia jumuiya za kimataifa, hapo awali aliushutumu Umoja wa Mataifa (UN), kuwa ni kijiwe cha kupiga soga kwani maamuzi ya Baraza la Usalama la UN yamekuwa hayana nguvu ya utekelezaji.
Trump alililaumu baraza hilo la UN kwa kutangaza kuizuia Israel kuendelea na ujenzi wa makazi ndani ya eneo la Palestina akisema yeye atakapoingia madarakani ataendeleza azma hiyo ya Israel.
NATO ilianzishwa mwaka 1949 wakati wa vita baridi kama muungano wa nchi za Ulaya ya Magharibi pamoja na Marekani kwa lengo la kukabiliana na Umoja wa Kisovieti (USSR).
Nchi za awali kujiunga na jumuiya hiyo zilikuwa ni Marekani, Ubelgiji, Uholanzi, Luxemburg, Ufaransa, Uingereza, Canada, Ureno, Italia, Norway, Denmark na Iceland huku mwaka 1952 nchi za Ugiriki,Uturuki na Ujerumani Magharibi zikifuatia.
Leave a comment