WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, amesema Serikali haitaingilia biashara za vyombo vya habari, ili wamiliki wake waendeshe shughuli zao kama ilivyo katika tasnia nyingine. Anaripoti Mwandishi Wetyu, Dar es Salaam … (endelea).
Nape ametoa kauli hiyo jana tarehe 15 Februari 2023, alipotembelea ofisi za Kampuni ya Mwananchi Communication Limited, akizungumzia Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya 2016, uliowasilishwa bungeni jijini Dodoma, hivi karibuni.
“Serikali haitaki kuingilia biashara ya vyombo vya habari. Inachotaka ni kuwa mlezi wa uhuru wa kujieleza na tunataka wamiliki wa vyombo vya habari, waendeshe biashara zao kama ilivyo kwa tasnia nyingine kama wanasheria, madaktari na wengine,” amesema Nape.
Waziri huyo amesema, Serikali imeamua kupelekwa muswada wa sheria ya habari bungeni, ili kuhakikisha vyombo vya habari vinafanya kazi zake kwa uhuru.
“Serikali itasimamia na kulinda uhuru wa kujieleza. Itahakikisha inafanya kila linalowezekana kulinda haki hiyo,” amesema Nape.
Nape amesema, baada ya muswada kusomwa bungeni kwa mara ya kwanza, utakabidhiwa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, ambapo itakuwa na jukumu la kuwaita tena wadau wa masuala ya habari kwa ajili ya kuwasikiliza, kisha itapeleka maoni ya wadau bungeni kabla ya Bunge kuanza kujadili maoni ya Serikali kuhusu sheria hiyo.
“Tulifanya mazungumzo ya kutosha kwa mwaka mzima kati ya serikali na wadau juu ya maboresho ya ile sheria, na yale tuliyokubaliana, tumeyazingatia kama serikali kwenye mapendekezo yetu bungeni,” amesema Nape.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri nchini (TEF), Bakari Machumu, amesema, mchakato kuelekea sheria hiyo, umekuwa wa majadiliano zaidi kati ya serikali na wadau waha habari.
“Kuna mapendekezo ambayo tuliyapeleka, yamesomwa. Kwa hiyo, tunachoangalia kwa sasa ni kwenda mbele kujua nini kimewekwa na kitajadiliwa kwa njia ipi” amesema Machumu.
Leave a comment