HATUA ya Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa CCM kukosoa vitendo vya baadhi ya Polisi kutumia nguvu katika kuwashughulikia wanasiasa, imemuibua Nape Nnauye, Mbunge wa Jimbo la Mtama. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kupitia ukurasa wake wa Twitter leo tarehe 13 Julai 2019, Nape amenukuu taarifa ya Dk. Bashiru iliyochapishwa na gazeti la mtandao la Mwananchi na kueleza kwamba, huyo ndiye Dk. Bashiru anayemjua.
Nape ameandika ‘Huyu ndio Dr. Bashiru Ally ninayemjua.”
Jana tarehe 12 Julai 2019 akizungumza katika ziara yake kwenye mji wa Kibaya Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara, Dk. Bashiru alisema Jeshi la Polisi likianza kutumia mabavu katika kutatua migogoro ya ndani, ni dalili ya kushindwa kuongoza nchi.
Dk. Bashiru amesema hakuna sababu ya Jeshi la Polisi kutumia mabavu, wakati wananchi wanatii sheria bila shuruti.
Aidha, Dk. Bashiru amesema nguvu ya ziada ni vyema ikatumika pale ambapo wananchi hawatii sheria.
Leave a comment