SERIKALI imezindua Kampeni ya ‘Tumewasikia Tumewafikia’ ambayo inawataka wakuu wa mikoa yote 26 na wakurugenzi wa halmashauri zote 184 nchini, kuandaa mikutano na vyombo vya habari ili kutangaza kwa wananchi kazi zinazofanywa na serikali. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma… (ndelea).
Hayo yameelezwa na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye wakati akizindua mikutano ya wakuu wa mikoa, wakurugenzi na vyombo vya habari jijini hapa jana Jumatano.
Alisema pamoja na kazi kubwa inayofanywa na serikali ya awamu ya sita wananchi bado hawana taarifa za kutosha.
Ameipongeza Idara ya Habari (Maelezo) kwa kuja na ubunifu huo na kuja kampeni hiyo ambayo wakuu wa mikoa pamoja na wakurugenzi wa halmashauri nchini wataitumia kuandaa mikutano na vyombo vya habari.
Alisema lengo lingine la kampeni hiyo ni kuongeza chachu ya mawasiliano kati ya wananchi na serikali yao kwa kuwa itatoa nafasi ya wakuu wa mikoa pamoja na wakurugenzi kueleza mambo ambayo yamefanywa.
“Serikali inatoa fedha nyingi za utekelezaji wa miradi mbalimbali hivyo wananchi wanayo haja ya kufahamu kodi zao zinafanya nini tunapozungumzia, maji, afya lazima waannchi wafahamu nini kinaendelea.
“Tumekuwa na utaratibu wa kufanya mikutano hii katika ngazi za wizara na taasisi hivyo mikutano hii itasaidia wananchi wa ngazi ya chini kabisa kufahamu nini serikali yao inafanya na huko ndiko pia serikali imekuwa ikipeleka kiasi kikubwa cha fedha katika utelezaji wa miradi mbalimbali,” alisema Nnauye.
Alisema pia kupitia program wananchi watapata fursa ya kueleza kile ambacho serikali yao imefanya na kimewanufaisha kwa namna gani.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo), Mobhare Matinyi, alisema lengo la kuanzishwa kwa kampeni hiyo ni kuwafikisha wananchi ngazi ya chini tarifa kuhusu kazi inayofanywa na serikali yao.
“Hivyo kampeni hii itasaidia kufikisha taarifa sahihi kwa wananchi kuhusu kile kinachofanywa na serikali yao na kuondoa ‘gap’ lililopo hivi sasa baina ya serikali na wananchi wake” alisema Matinyi.
Hata hivyo, alisema kampeni hiyo baada ya jana itakwenda katika mikoa yote na halmashauri zake zote 184 nchini ambapo awamu ya kwanza itakuwa ni mikoa ya Dodoma, Morogoro, Pwani na Dar es Saalam.
Leave a comment