Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Makala & Uchambuzi Namungo wametushangaza, ila Manyama ameshangaza zaidi
Makala & UchambuziMichezo

Namungo wametushangaza, ila Manyama ameshangaza zaidi

Edward Charles Manyama
Spread the love

DIRISHA dogo la usajili kwa klabu za Ligi Kuu Tanzania Bara na ligi daraja la kwanza, limefungwa tarehe 15 Januari 2021, huku baadhi ya timu zikiendelea kujiimarisha kupitia usajili huo, lakini usajili ulioshangaza waliowengi ni wa beki wa pembeni wa Namungo FC, Edward Charles Manyama ambaye kujiunga na Ruvu Shooting kama mchezaji huru mara baada ya kuisha kwa mkataba wake na klabu hiyo. Anaandika Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea). 

Unaweza ukaonekana kama uhamisho wa kawaida kwa mchezaji kutoka timu moja kwenda nyingine, lakini Manyama kuondoka kwake Namungo na kujiunga na Ruvu shooting umeshangaza na kufikilisha.

Namungo wanaweza wakatoa majibu ya maswali muhimu katika uhamisho huo, kubwa likiwa, kwanini wanaruhusu mchezaji aina ya Manyama kumaliza mkataba wake na kuondoka kama mchezaji huru wakati timu bado ipo kwenye michuano ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Manyama amekuwa chaguo la kwanza katika kikosi cha Kocha, Hemed Moroco wakati wa michezo ya Namungo ya Ligi Kuu Bara na ile ya kimataifa, ambapo hivi karibuni wana mchezo dhidi ya Costo de Agosto ya Angola kwenye kombe la shirikisho na wakifanikiwa kuwaondoa watafuzu kwenye hatua ya makundi.

Isingekuwa usajili wa kustua kama Manyama angeondoka Namungo, timu inayoshiriki michuano ya kimataifa na kujiunga na Simba, Azam FC au Yanga ambazo zinanafasi ya kucheza michuano mikubwa kama hiyo.

Lakini hili jambo la mchezaji huyu kujiunga na Ruvu Shooting limeacha maswali mengi kutokana na timu hiyo kutokuwa na ushawishi mkubwa wa kifedha kuliko, wala timu hiyo haiwezi kumpa ushindani wa kulinda kiwango chake ili kuweza kurudi tena kwenye timu ya Taifa.

Ikumbukwe Manyama kwa sasa yupo kwenye kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania kilichopo nchini Cameroon, ambacho leo 19 januari 2021 kinashuka dimbani kwenye mchezo wake wa kwanza kundi D, dhidi ya Zambia.

Manyama amekuwa mchezaji muhimu ndani ya kikosi cha Namungo toka walipopanda Ligi Kuu Tanzania Bara kwenye msimu wa 2019/20 na kufanikiwa kumaliza Ligi wakiwa nafasi ya nne nyuma ya klabu za Simba, Yanga na Azam FC.

Kama kweli Manyama anajua ukubwa wa kipaji chake kwa sasa asingekuwa na haraka ya uhamisho huo wakati wakati anajua anakwenda kwenye michuano mikubwa kama CHAN, napengine ingekuwa nafasi nzuri kwake kutumia michuano hiyo kama soko la kujiuza.

Edward Charles Manyama

Leo hii kwenye Ligi yetu tunaona fahari kuwa na wachezaji kama Lary Bwalya raia wa Zambia na Thadeo Lwanga kutoka Uganda, ambao wote wanacheza Simba, bila ya kukumbuka kuwa hao wote ni matunda ya michuano ya CHAN iliyofanyika mara ya mwisho.

Ni ngumu sana kwa mchezaji mwenye malengo ya kufika mbali kuikacha timu inayoshiriki mashindano ya kimataifa kwa ngazi ya klabu barani Afrika na kujiunga na timu inayoshiriki Ligi Kuu pekee.

Tukumbuke hata safari ya Mbwana Samatta kucheza soka la kulipwa barani Ulaya ilianzia katika michuano kama hii ya ngazi ya klabu ndani ya bara la Afrika ambapo Simba walicheza na TP Mazembe kisha mabosi wa timu hiyo wakavutiwa naye na leo dunia nzima inamtambua.

Manyama amepishana na fursa ambayo inaweza isije tena kwa klabu aina kama Namungo kushiriki tena michuano ya kimataifa kutokana na timu kama za Yanga na Azam FC ambazo hazipo kwenye michuano hiyo kuwekeza zaidi ili waweze kufanya vizuri kwenye msimu huu na kurudi kwenye michuano hiyo.

Mategemeo ya wengi yalikuwa kumuona kijana huyo akichezea timu kubwa hata za ndani ya nchi kutokana na umahili wake ndani ya uwanja sio tu kwenye kuzuia, na atakuwa na uwezo mkubwa wa kufunga na ameshafanya hivyo kwenye mechi kubwa.

Achana na mchezaji huyo tu, lakini hata Namungo wanatushangza kwenye jambo hili, kwa kukubali Manyama kuondoka kwenye timu hiyo akiwa kama mchezaji huru mara baada ya mkataba kumaliza katikati ya msimu.

Viongozi wa Namungo wanapaswa kufahamu kuwa timu yao inahitaji kuwepo wachezaji wenye uwezo aina kama ya Manyama kutokana na michuano wanayoshiriki, na ndio maana tunaona hata barani ulaya klabu zinavyoangaika kuwapa mikataba mirefu wanaonekana kuwa muhimu na mchango mkubwa kwenye kikosi.

Sitaki kuamini kama Namungo walishindwa kumbakisha Manyama kwa ghalama yoyote kiasi cha kwenda Ruvu Shooting, klabu ambayo ukilinganisha nguvu ya kiuchumi haiwezi kufanana na klabu aliyotoka.

Kitendo cha Namungo kumwachia Manyama kutimkia Ruvu ni kurudia kosa kama walilofanya kwa Reliant Lusajo aliyekuwa mfungaji wao bora kwenye kikosi chao msimu uliomalizika kwa kumuachia kwenda KMC na baadae timu ikaonekana kutopata mabao mengi kwenye baadhi ya michezo ya ligi kuu.

Namungo wanapaswa kujua kwamba kuwa na wachezaji wenye kiwango kama cha Manyama ni muhimu kwa ustawi wa timu na hata kama anaondoka anapaswa kuondoka kwa kuuzwa ili timu iweze kutengeneza fedha lakini sio kuondoka bure.

Ni ngumu kuamini kuwa mchezaji kama huyo ambaye mwenye kipaji kikubwa kiasi cha kumvutia kocha wa timu ya Taifa, Ettiene Ndayilagije kumuacha Mohammed Hussein kwenye kikosi kilichoenda CHAN, na kumjumuisha yeye kwenye timu hiyo kusikia anaondoka bure.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Miaka 28 watumishi UDSM yaliwa na nzige, madumadu

Spread the loveGEORGE Francis anasikitika; anatembea akiwa na mawazo mengi, hajui la...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nimekumbuka Samia wa miaka 3 iliyopita

Spread the loveWAKATI naandaa makala ya safu hii wiki hii, nimejikuta nakumbuka...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Hakuna fedha za Rais

Spread the loveKUNA mambo machache mazuri ya kujifunza kutoka kwa Margaret Thatcher,...

error: Content is protected !!