NDIYO hivyo. Kikosi cha Namungo FC kimepoteza mchezo wa pili wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Pyramids kutoka nchini Misri kwa mabao 2-0. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Sakaam … (endelea).
Mchezo huo wa kundi D, ulipigwa kwenye Uwanja wa Benjamini Mkapa jijini Dar es Salaam majira ya saa 10 kamili jioni.
Pyramids ambao walikuwa wageni kwenye mchezo huo, walitawala kwa kiasi kikubwa katika dakika 90 za mechi hiyo, walipata bao la kwanza kwa njia ya mkwaju wa penalti kwenye dakika ya 71 lililofungwa na Ramadan Sobhi.
Mara baada ya bao hilo, Namungo walionekana kuamka kwa kupeleka mashambulizi kwenye lango la Pyramids huku juhudi zao hazikuzaa matunda na dakika 13 baadae Omar Gaber alipachika bao la pili kwenye dakika ya 84, bao lilidumu mpaka mwisho wa mchezo huo.
Kwa matokeo hayo Pyramids inaendelea kusalia kileleni baada ya kuibuka na ushindi kwenye michezo yake miwili hivyo kujikusanyia pointi sita, huku Namungo ikishika nafasi ya nne ikiwa haina pointi.
Mchezo ujao Namungo itasafiri mpaka nchini Zambia kuvaana na Nkana Red Devil ambao muda mfupi ujao watashuka dimbani dhidi ya Raja Casablanca.
Katika mchezo wa kwanza Namungo ilipoteza kwa bao 1-0, dhidi ya Raja Casablanca kwenye mchezo uliopigwa nchini Morocco.
Leave a comment