NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Mwaikabe Waitara, amewataka wakandarasi wazawa nchini kujiepusha na vitendo vya rushwa wakati wa kuomba na kutekeleza zabuni za miradi ya serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Amesema, vitendo vya rushwa kwenye zabuni, husababisha utekelezaji wa miradi hiyo, kufanyika chini ya kiwango na wakati mwingine kushindwa kabisa kumalizika.
Naibu waziri huyo ametoa kauli hiyo, jijini Mwanza wakati akifunga mkutano wa nne na wa mwisho wa mashauriano na wadau wa sekta ya ujenzi kwa mwaka 2021.
Mkutano huo wa wadau wa sekta ya ujenzi, uliandaliwa na Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB).
Katika mkutano huo, Waitara amesisitiza miradi inayotolewa kwa wakandarasi wazawa itekelezwa kwa ubora na viwango kama ilivyo katika mikataba, ili thamani ya fedha iweze kuonekana.
Amesema, nia ya serikali ni kuendelea kuwapa miradi mingi wakandarasi wazawa, lakini lazima waoneshe uwezo wao wa kutekeleza miradi waliyopewa.
Alisema, “nawasihi msitoe rushwa katika kuomba miradi, mshirikiane na muache ubinafsi, ili muweze kupata miradi mikubwa na kuitekeleza kwa pamoja.”
Aliongeza, “kama kuna changamoto, mikutano mikubwa kama hii ndio mahali sahihi ya kuzungumzia utatuzi wa changamoto hizo.”
Amesema, ni muhimu kwa wakandarasi wazawa kushiriki miradi mikubwa inayofanywa na wakandarasi kutoka nje, ili kuwasaidia kupata uzeofu na ujuzi wa kutosha.
Amesema, hatua hiyo itasaidia, wakati miradi hiyo inapohitaji kufanyiwa ukarabati, kazi hiyo yaweza kufanywa na wakandarasi wa ndani badala ya wakandarasi wa kigeni.
Kwa upande wake, Msajili wa CRB, Rhoben Nkori, amemuambia Naibu Waziri Waitara kuwa Bodi yake itafanya majumuisho ya maazimio yote ya mikutano minne iliyofanyika na kuyawasilisha wizarani kwa ajili ya kupatiwa utatuzi wa changamoto na kuona namna bora ya kuwawezesha wakandarasi hao hasa katika miradi inayotarajiwa kutangazwa.
Alisema, “mheshimiwa Naibu Waziri, jumuiya ya wakandarasi inapenda kukushukuru kwa kushirikiana nasi katika mikutano yetu miwili ya Arusha na hapa Mwanza, na kwa niaba ya wenzangu napenda kukuahidi kuwa maelekezo yako yote uliyotupatia kwenye vikao hivi viwili tunakwenda kuyafanyia kazi.”
Mkutano huo, ulihudhuriwa na wadau takribani 1,366 wa sekta ya ujenzi katika mikoa ya Arusha, Mbeya, Dar es Salaam na Mwanza. Kati yao, wakandarasi walikuwa 1,035 na wengine waliosalia siyo wakandarasi.
Leave a comment