WILLIAM Tate Ole Nasha, aliyekuwa Mbunge Ngorongoro na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-Uwekezaji nchini Tanzania, amehitimisha safari yake ya mwisho hapa duniani kwa mwili wake kuzikwa nyumbani kwake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Maziko hayo yamefanyika leo Jumamosi, tarehe 2 Oktoba 2021, nyumbani kwake kijiji cha Osinoni kata ya Kakesyo wilayani Ngorongoro, Mkoa wa Arusha na kuhudhuriwa na Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kwa niaba ya Rais wa nchi hiyo, Samia Suluhu Hassan.
Ole Nasha alifikwa na mauti usiku wa tarehe 27 Septemba 2021, akiwa nyumbani kwake, jijini Dodoma.
Akizungumzo katika shughuli ya maziko hayo, Majaliwa amesema, kifo cha Ole Nasha ni pigo kubwa kwa Serikali, Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bunge pamoja na kwa wanafamilia na wananchi wa Ngorongoro.
Waziri mkuu amesema, Rais Samia anawataka Watanzania waenzi mambo mazuri yote aliyoyafanya marehemu Ole Nasha ili jamii aliyokuwa anaiongoza inufaike. “Marehemu amefanya mambo mengi na ametoa mchango wa hali ya juu kwa Serikali.”
Amesema jambo la muhimu kwa sasa ni kuendelea kumuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema.
“Mke wa marehemu, watoto, ndugu, jamaa na wabunge nawaombea kwa Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu.”
Kwa upande wake, Waziri Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu –Uwekezaji, Geofrey Mwambe amesema Serikali hususani Ofisi ya Waziri Mkuu imepata pigo kubwa kwa kumpoteza mpiganaji kwa sababu marehemu Ole Nasha alikuwa mtumishi hodari.
Mazishi hayo yamehudhuriwa na Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai, Spika wa Bunge la Afrika Mashariki, Dk. Martin Ngoga, viongozi wa Serikali, wabunge pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali.
Leave a comment