NAHODHA wa klabu ya Yanga, Lamine Moro amewashangaa wanaodai kuwa timu hiyo imekata tamaa na ubingwa wa Ligi kuu Tanzania Bara, baada ya kumtimuliwa kwa aliyekuwa kocha wa Cedric Kaze. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Beki huyo wa kati ameyazungumza hayo leo, mbele ya waandishi wa habari katika mkutano wao uliofanyika Makao Makuu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuelekea mchezo wa kesho wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya KMC.
Lamine amesema kuwa wakati ligi hiyo imesimama yalizungumzwa mambo mengi, baada ya kufukuzwa kocha wao, Cedric Kaze huku akisisitiza kuwa jambo hilo ni kawaida kutokea kwenye mpira.
“Tulikuwa mapumziko ya muda mrefu na sasa ligi imerudi tena nafikiri tupo tayari, ukiangalia kabla ya kusimama kwa Ligi watu walivyokuwa wanaongea kuwa wamefukuza kocha wao wakati kwenye mpira vitu hivi vinatokea,” alisema Lamine.
Aidha nahodha huyo alisema, kuna baadhi ya watu walisema wemekata tamaa, lakini wao wamejipanga kwa mchezo wa kesho na hajawahi kucheza mchezo rahisi toka alipofika Tanzania.
Kwa upande wa Kocha Mkuu wa kikosi hicho, Juma Mwambusi alisemaa, wanacheza mchezo huo wakiwa nyumbani na watapambana kupata pointi tatu.
“Tunacheza tukiwa nyumbani, wanayanga wanatarajia kupata matokeo mazuri, tutapambana kupata pointi tatu muhimu na hilo ndiyo jambo muhimu,” alisema kocha huyo.
Kwenye mchezo wa mzunguko wa kwanza waliocheza kwenye dimba la CCM Kirumba, Yanga ilifanikiwa kuondoka na ushindi wa mabao 2-1.
Leave a comment