MWILI wa Zacharia Hans Pope, mjumbe wa bodi ya wakurugenzi wa timu ya Simba nchini Tanzania utaagwa kesho Jumatatu, tarehe 13 Septemba 2021, ukumbi wa Karimjee, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hans Pope, ambaye pia alikuwa mjumbe wa kamati ya sharia, hadhi na madaraka ya wachezaji alifariki dunia usiku wa Ijumaa tarehe 10 Septemba 2021, katika Hospitali ya Agha Khan jijini Dar es Salaam jijini humo alipokuwa akipatiwa matibabu.
Ratiba iliyotolewa na mabingwa wa ligi kuu Tanzania bara 2020/21, Simba inaonesha mwili wa Hans Pope utazikwa kijijini kwao, Kihesa Mkimbizi mkoani Iringa.
Mbali na kujihusisha na masuala ya michezo, Hans Pope aliyekuwa mwenyekiti wa kamati ya usajili wa Simba aliwahi kuwa Luteni wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), akiwa miongoni mwa waliotaka kufanya jarabio la kumpindua Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, lakini wakashindwa.
Hatua hiyo, ilimfanya Hans Pope na wenzake kutupwa gerezani hadi mwaka 1995 walipokuja kuachiwa na Rais wa wakati huo, Ali Hassan Mwinyi.
Leave a comment