ROBERT Fuller (24), mmarekani mweusi amekutwa ananing’inia kwenye mti baada ya kunyongwa katika mji wa Palmdale, Califonia nchini Marekani. Inaripoti mitandao ya kimataifa…(endelea).
Familia ya Robert imetaka maelezo kutoka kwa jeshi la polisi jijini humo kuhusu kifo cha ndugu yao. Kifo hicho kimebainika ikiwa ni siku mbili baada ya Rayshard Brooks (27) kupigwa risasi na polisi wa Atlanta na kuuawa, pia wiki tatu baada ya polisi wa Minnesota kumuua George Floyd (46).
Nchini humo, maandamano kupinga ubaguzi wa rangi yameendelea kushika kasi. Mwili wa Robert umebainika Jumamosi ya mwisho wa wiki. Taarifa za awali za polisi jijini humo zinadai, Robert anaweza kuwa amejinyonga mwenyewe.
Hata hivyo, polisi wamesema wanasubiri ripoti kamili. Familia ya Robert imehoji ‘anawezaje kujinyonga wakati hakuna mvutano wowote?’
“Kila wanachotueleza hakielekeani na ukweli wowote,” amesema dada yake Robert, Diamond Alexander ambaye ni miongoni mwa waandamanaji wanaopinga ubaguzi wa rangi kwenye maandamano yanayoendelea sasa nchi humo.
Amesema, wamekuwa wakipokea maelezo tofauti kutoka kwa polisi tofauti kuhusu kifo cha ndugu yao na kwamba, hawaamini kama Robert alijiua mwenyewe.
“Tumekuwa tukipokea majibu tofauti. Ukikutana na polisi mwingine anakupa jibu tofauti, sasa tunachotaka ni kujua ukweli. Kaka yangu hajajinyonga, hapana hakujinyonga,” amesema Diamond.
Leave a comment