MWANDISHI wa Habari mwandamizi wa gazeti la Nipashe kutoka kampuni ya IPP Media, Richard Makore amefariki dunia katika ajali iliyoua watu saba eneo la Ibanda Kona, Kata ya Kasamwa wilayani Geita mkoani Geita. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Ajali hiyo ilitokea jana tarehe 7 Machi 2023 saa 10 jioni baada ya gari la Sheraton lililotokea Mwanza kwenda Ushirombo wilayani Geita kupasuka tairi ya mbele na kupinduka.
Taarifa za kifo cha Makore zimethitishwa na Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa habari ya Mkoa wa Mwanza (MPC), Edwin Soko ambaye ameeleza kuwa mwili wa Makore umehifadhiwa katika hospitali ya Geita.
“MPC inasikitika kutangaza kifo cha Mwanachama wake Richard Makore kilichotokea jana lwenye ajali ya gari (Min bus) iliyotokea Mkoani Geita. Makore alikuwa anafanya kazi na Gazeti la Nipashe Mwanza na pia ni Mwanachama hai wa MPC.
“Kwa sasa mwili wake upo kwenye chumba cha kuhifadhi Maiti hospitali ya Geita. MPC inawaomba wanachama wake wote kuwa watulivu kwenye wakati huu mgumu kwetu. Bwana alitoa na Bwana ametwaa jina lake lihidimiwe,” imesema taarifa hiyo.
Awali akizungumzia ajali hiyo Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Berthaneema Mlay amesema majeruhi waliwahishwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa kwa matibabu zaidi.
POLENI WAFIWA KWA AJALI ILIYOTOKEA GEITA