MGOMBEA wa nafasi ya Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kunje Ngombale Mwiru amewapagawisha wabunge baada ya kuwaahidi kupunguza idadi ya vikao na kuongeza posho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mwiru ambaye ni mtoto wa aliyekuwa mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Ngombale Mwiru, ametoa kauli hiyo leo tarehe 1 Februari, 2022 wakati akiomba kura kwa wabunge ili achaguliwa kuwa Spika wa Bunge hilo.
Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa viti maalumu – CCM, Mwanaisha Ng’azi Ulenge aliyemtaka kueleza changamoto tatu zinazohusiana na kazi za Bunge na namna ya kuzitatua.
Mwiru ambaye ni mgombea kutoka Chama cha Sauti ya Umma (SAU), ametaja changamoto hizo kuwa ni kuwapatia wabunge usafiri ili kufika kwa urahisi wa kufika kwenye majimbo yao bila changamoto.
“Nitahakikisha kila mbunge namkabidhi gari lenye uhakika bila mkopo. Kwa sababu nchi yetu imejaliwa rasilimali nyingi hatuna sababu ya kupeana madeni, mbunge akipewa madeni ya kulipia gari atashindwa kuhudumia wananchi.
“Changamoto ya pili ni vikao… vimekuwa vingi, tunahitaji viwe vichache lakini nitaongeza posho ili muende vijijini mkahudumie Watanzania,” amesema.
Aidha, ameeleza kuanzisha kikosi kazi cha kufuatiilia wabunge watoro majimbo mwao.
“Nitaanzisha kitengo cha task force cha kumfuatilia mbunge mmoja mmoja ili kuhakikisha wanafika majimbo kutatua changamoto za wapiga kura,” amesema na kushangiliwa kwa nguvu na wabunge.
Pamoja na mambo mengine, mgombea huyo licha ya kuhama vyama zaidi ya vitano, amesema atalisimamia Bunge kwa uweledi.
Leave a comment