MWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Njelu Kasaka amefariki dunia katika Hospitali ya Rufaa Mbeya alipokuwa akipatiwa matibabu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya … (endelea).
Kasaka aliyekuwa miongoni mwa Wabunge 55 walioasisi Kundi la G55 lililotaka kuundwa Serikali ya Tanganyika mwaka 1993, amefikwa na mauti usiku wa kuamkia leo Ijumaa tarehe 3 Julai 2020 katika Hospitali ya Rufaa Mbeya.
MwanaHALISI ONLINE limezungumza na Masache, mtoto wa wa pili wa marehemu ambaye amesema, “Baba amefariki usiku wa kuamkia leo na tatizo lililokuwa linamsumbua ni tatizo la moyo.”
“Wakati ananedelea na matibabu katika hospitali akapata mshituko wa moyo uliosababisha kufariki dunia,” amesema Masache.
Amesema, msiba uko nyumbani kwake, Chunya mkoani Mbeya, “na mazishi yatakuwa Jumapili (tarehe 5 Julai,2020).”
Masache amesema, baba yake ameacha watoto saba na mjane mmoja.
Kasaka ambaye amepata kuwa mbunge, waziri na mkuu wa mkoa, alijitoa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) mwaka 2015 na kujiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kugombea ubunge jimbo la Lupa.
Hata hivyo, alishindwa na mgombea wa CCM, Victor Mwambalaswa.
Mapema mwaka 2019, Kasaka alizindua kitabu chake alichokiita ‘Njelu Kasaka: Maisha, Siasa na Hoja ya Tanganyika-G55.”
Katika moja ya maelezo kwenye kitabu hicho anaeleza alivyoingia bugeni kwa mara ya kwanza.
“Niliingia Bungeni Novemba, 1990 baada ya kushinda katika uchaguzi wa Ubunge jimbo la Chunya uliofanyika Oktoba 28 mwaka huo.”
“Jimbo la Chunya lilianzishwa mwaka 1965 na mbunge wa Kwanza alikuwa Raphael Anthony Kinyonga. Kwa kumbukumbu zilizopo mimi nilikuwa mbunge wa nne kushika nafasi hii katika jimbo hili,” anasema Kasaka katika kitabu hicho
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online & MwanaHALISI TV kwa habari zaidi
Leave a comment