MWANTUM Mussa Sultan, amekuwa mwanamke wa kwanza kujitosa katika mchakato wa kuomba kuteuliwa na Chama cha Mapinduzi (CCM), kugombea Urais wa Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Mwantuma amechukua fomu Leo Ijumaa tarehe 19 Juni 2020 katika Ofisi za CCM visiwani Zanzibar zilizoko Kisiwandui na kukabidhiwa Cassian Gallo’s, katibu wa Kamati Maalumu ya NEC Idara ya Oganaizesheni Zanzibar.
Mara baada ya kukabidhiwa, Mwantumu amesema, amefanya hivyo ili kutoa hamasa kwa wanawake kujitosa katika kinyang’anyiro hicho, kutimiza sera ya haki sawa kwa wote.
“Nimekuja kuwapa hamasa kina mama wenzangu ili na sisi wanawake tujitokeze. Tuko wengi bila wanawake hakuna kitu, tujitokeze kuchukua fomu tupate asilimia yetu tuliyoomba ya hamsini hamsini,” amesema Mwantumu.
Mwantumu anakuwa kada wa 11 wa CCM kujitosa katika kinyang’anyiro hicho, tangu zoezi hilo la siku 15 lifunguliwe Jumatatu ya tarehe 15 Juni 2020.
Zoezi hilo linaloenda sambamba na utafutaji wadhamini 250 kwa kila mgombea, linatarajiwa kufika tamati tarehe 30 Juni mwaka huu.
Mwantuma amechukua fomu akitanguliwa na Waziri wa Maji, Profesa Makama Mbarawa.
Wengine waliokwisha chukua fomu ni; Mbwana Bakari Juma alikuwa mtu wa kwanza kufungua dimba hilo.
Balozi Ali Abeid Karume ambaye ni mtoto wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Hayati Abei Aman Karume kisha akafuatiwa na Mbwana Yahaya Mussa ambaye mpaka sasa ndiye mwanachama kijana aliyejitosa kuchukua fomu.
Mtaalamu wa uchumi aliyewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi katika tawala zilizipita visiwani Zanzibar, Omary Sheha Mussa alikuwa wan ne kuchukua fomu.
Watano katika kunyany’anyiro hicho alikuwa, Waziri wa Ujenzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dk. Hussein Mwinyi ambaye ni mtoto wa Rais mstaafu wa Zanzibar na Tanzania, Ali Hassan Mwinyi.
Shamsi Vuai Nahodha, Waziri Kiongozi Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) alikuwa wa sita kuchukua fomu kasha akafuatia Mohammed Jaffar Jumanne, Mkurugenzi wa Ushindani wa Biashara Halali Zanzibar.
Wanane, alikuwa Mohammed Hijja Mohammed na wa tisa akawa, Balozi Meja Jeneral mstaafu, Issa Suleimani Nassor.
Leave a comment