MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imeamuru gazeti la kila wiki la MwanaHALISI ambalo lilifungiwa na serikali, liendelee kuchapishwa. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu, tarehe 30 Julai, ofisini kwake, Kinondoni, mkurugenzi wa kampuni ya Hali Halisi Publishers Limited (HHPL), Saed Kubenea amesema, mahakama imeridhia MwanaHALISI kurudi tena mtaani, kufuatia mamlaka iliyoifungia kutokuwa na nguvu za kisheria.
MwanaHALISI lilifungiwa na serikali, tarehe 19 Septemba 2017, kwa madai kuwa limekuwa “likiandika habari za uongo, kejeli, upotoshaji, uchochezi na zinazolenga kuwafanya wananchi waichukie serikali yao.”
Hukumu ya kuruhusiwa kuchapishwa kwa MwanaHALISI, imetolewa na Jaji Beatrice Mutungi, tarehe 24 Julai mwaka huu.
Amri ya kufungia MwanaHALISI, ilitolewa na aliyekuwa naibu waziri wa habari, utamaduni, sanaa na michezo, Anastazia Wambura, tarehe 19 Septemba2017.
Kubenea amesema, mahakama imethibisha kuwa gazeti lake, halikuwa na makosa; mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) na naibu waziri Wambura, walijichukulia mamlaka wasiyokuwa nayo.
Amesema, hukumu hiyo imedhihirisha kuwa wapo watendaji ndani ya serikali wanaotumia mamlaka walizopewa “kushughulikia wenzao” kwa maslahi yao binafsi.
Amesema, kutokana na hali hiyo, wanatarajia gazeti hilo kuingiza mtaani Jumatano ya tarehe 8 Agosti na kwamba wamepanga kumchukulia hatua za kisheria Wambura.
Leave a comment