MBUNGE wa Muheza, Hamis Mwijuma (CCM) maarufu kama Mwana FA amesimulia namna alivyonusurika kifo katika ajali iliyotokea katika eneo la Mkambarani mkoani Morogoro. Anaripoti mwandishi wetu, Morogoro … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kufikishwa katika hospitali ya mkoa wa Morogoro leo tarehe 30 Agosti, 2021, Mwana Fa amesema ajali hiyo ilitokea baada ya gari alilokuwa akisafiria kugongana na gari ndogo aina ya Toyota Crown iliyokuwa ikijaribu kulipita gari lake wakati akitoka Dar es Salaam kuelekea jijini Dodoma.
“Ndani ya gari yangu tulikuwa watu wawili, mimi na dereva wangu, tulitoka Muheza tukapita Msoga kwa Rais mstaafu ambaye alikuwa amefiwa na mtoto wa kaka yake. Baada ya maziko tukawa tunatoka kuelekea Dodoma.
“Tulipofika sehemu inayoitwa Kingolwira… huwa kuna malori mengi… kuna mtu akawa ana-overtake, alikuwa spidikuwa sana ni kati ya 140 hadi 160. Tulikuwa tunamuona anakuja lakini tunashukuru tumetoka salama. Mimi nina maumivu kifuani na mkono wa kushoto,” amesema.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mororgoro, Fortunatus Musilim amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo iliyotokea muda was aa mbili usiku.
“Hata hivyo Mheshimiwa Mbunge alitumia gari lake kuwapeleka majeruhi katika hospitali ya Mkoa,”amesema.
Kamanda Musilim amesema, watu wengine wawili waliokuwa kwenye Crown walipata michubuko kadhaa na wako salama.
Leave a comment