KUELEKEA mchezo wa kufuzu kwa michuano ya Kombe la Dunia dhidi ya Benin mlinzi wa kati wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars,’ Bakari Mwamnyeto na beki wa kulia Shomari Kapombe huenda wakaukosa mchezo huo kutokana na kukabiliwa na majeruhi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo wa kundi J, utapigwa siku ya Alhamisi Oktoba 7, 2021 majira ya saa 10 jioni, kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.
Akitoa taarifa ya wachezaji hao ikiwa siku moja toka kikosi hiko kuingia kambini, Meneja wa Taifa Stars Nadir Haroub, amesema kuwa idadi kubwa ya wachezaji wameshaingia kambini isipokuwa wachezaji wawili wa kimataifa Mbwana Samatta ambaye aliwasili jana saa 5 usiku akitokea Ubelgiji na Simon Msuva ambaye amewasili leo nchini majira ya asubuhi akitokea nchini Morocco.
“Leo tumeanza sehemu yetu ya kwanza ya mazoezi, kiujumla wachezaji wamesawali kasoro Mbwana Samatta ambaye ataingia leo (jana) saa 5 usiku na Simon Msuva ataingia kesho asubuhi,”alisema Meneja huyo.
Taifa Stars inaingia kwenye mchezo huo huku wakiwa vinara kwenye kundi J, wakiwa na pointi nne baada ya kucheza michezo miwili.
Aidha Meneja huyo alifunguka hali za wachezaji mara baada ya kuwasili kambini na kufunguka kuwa, wachezaji watatu walikuwa na maumivu ambao ni Mwamnyeto, Kapombe pamoja na Erasto Nyoni ambao walipata majeruhi hao wakiwa kwenye klabu zao.
Mara baada ya mchezo huo utakaopigwa Oktoba 7 2021, kikosi cha Stars kitasafiri kuelekea kwenye mchezo wa marudiano nchini Benin utakaopigwa Oktoba 10, 2021.
Leave a comment