KAMATI ya Maadili ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemfungia miaka mitano kujihusisha na mpira wa miguu, Makamu Mwenyekiti wa klabu ya Yanga, Frederick Mwakalebela, baada ya kuvishutumu vyombo vinavyosimamia Ligi Kuu Bara kuwa wanaihujumu Yanga. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya kufungiwa kwa kiongozi huyo imetolewa hii leo tarehe 2 Aprili, 2021 na idara ya mawasiliano ya TFF.
Kamati hiyo, imesema Mwakalebela alilalamikiwa tarehe 19 Februari, 2021, baada ya kuitisha mkutano na waandishi wa Habari na kudai kuwa TFF, Bodi ya Ligi na kamati ya uendeshaji na usimamizi wa Ligi, inahujumu klabu ya Yanga madai ambayo alishindwa kuthibitisha mbele ya kamati.
Katika hatua nyingine makamu mwenyekiti huyo, ametozwa faini ya Sh. 5,000,000, kwa kosa la kutoa maneno ya uchochezi kwa wanachama wa klabu ya Yanga dhidi ya vyombo vinavyosimamia mpira nchini.
Aidha taarifa hiyo, imesema kosa la pili, Mwakalebela alilalamikiwa kwa kutoa taarifa za uongo kuhusu mkataba wa mchezaji Bernard Morrison na klabu ya Simba mbele ya waandishi habari huku kitendo hiko kikiwa kinyume na sheria.
Katika shtaka hilo kamati ilimtia hatiani Mwakalebela, kwa kosa hilo na kumpa onyo kwa kutotenda kosa hilo katika kipindi cha miaka mitano na kutozwa faini ya Sh. 2,000,000.
Adhabu ya kumfungia kwa miaka mitano, kiongozi hiyo imetolewa kwa kuzingatia kifungu cha 73(4) cha kanuni za maadili toleo la 2013.
Leave a comment