Friday , 29 March 2024
Home Habari Mchanganyiko Mvua yaelezwa chanzo ajali ya treni iliyoua, kujeruhi
Habari MchanganyikoTangulizi

Mvua yaelezwa chanzo ajali ya treni iliyoua, kujeruhi

Spread the love

WATU watatu, wamefariki dunia na wengine 66, kujeruhiwa katika ajali ya treni iliotokea jana Jumamosi jioni tarehe 02 Januari 2021, maeneo ya Kigwe Wilayani Bahi mkoani Dodoma. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).

Ajali hiyo ilihusisha Tren B 17 yenye kichwa namba 9004, iliyokuwa ikitokea Dar es Salaam kwenda Tabora, Kigoma Mwanza na Mpanda.

Akizungumza katika eneo la ajali mara baada ya kufanya ziara ya kukagua eneo la tukio, Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene, alisema moja ya sababu inayoweza kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mvua kubwa zinazoendelea kunyesha hivi sasa.

Simbachawene, alisema, kutoka na mvua zinazoendelea kunyesha zimesababisha uwepo wa michanga pamoja tope kwenye njia ya treni ambayo inaweza kuwa ndiyo sababu kuu ya kutokea kwa ajali hiyo.

Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk. Binilith Mahenge akizungumzia tukio hilo, alisema sababu kubwa ya ajali hiyo ni mvua kubwa iliyonyesha katika eneo hilo na kusafisha msingi wa njia ya treni hali ambayo imesababisha reli kukosa nguvu.

“Mvua kubwa sana zimenyesha katika eneo lile, hali ambayo imesababisha msingi wa reli kuondolewa na maji ya mvua hali iliyosababisha reli kuinuka juu ndiyo hofu yetu kuwa reli haikuwa na nguvu ya kuhimili mzigo na kusababisha ajali hii”alifafanua Dk. Mahenge.

Dk. Mahenge alisema zaidi ya abiria 400, walisafirishwa na mabasi zaidi ya 20, kupelekwa Manyoni Mkoa wa Singida kuendelea na safari katika maeneo waliyokuwa wanaenda.

“Abiria wote tayari tumeshawaondoa katika eneo la ajali na kazi iliyobaki ni kunyanyua yale mabehewa na mitambo tayari imeshaandaliwa kwa ajili ya kwenda kuondoa yale mabehewa” alieleza Dk. Mahenge

Aidha, katika taarifa iliyotolewa na kitengo ya Mawasiliano cha Shirika ya Reli Tanzania (TRC), ilieleza Treni hiyo iliwasili jijini Dodoma majira ya saa 9:15 Alasiri na kuondoka majira ya 11:40 jioni kuelekea mikoa ya Tabora, Shinyanga, Kigoma, Mwanza na Mpanda.

 

Ambapo iliwasili saa 12:25 katika stesheni ya Kigwe Wilayani Bahi na kuondoka 12:27 kuendelea na safari yake ambapo ndipo ajali hiyo ilipotokea.

Taarifa hiyo pia ilieleza kuwa  ajali hiyo ilihusisha Treni B 17, yenye mabehewa 12, ikiwa na abiria 720.

Mabehewa sita kati ya 12, ndiyo yaliopata ajali baada ya kupinduka na kusababisha vifo vya watu watatu na majeruji 66 ambao wamefikishwa katika hospitali ya rufani ya mkoa wa Dodoma (General Hospital) huku wengine wakiendelea na matibabu katika hospitali ya Bahi.

“Mpaka sasa watu waliopoteza maisha katikia ajali hiyo ni watatu akiwemo mtoto mmoja na watu wazima wawili wanawake ”ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Mabehewa yaliyopata ajali ni TCB 3603 la kwanza kutoka kichwa cha treni, TCB 3612, la pili kutoka kichwa cha treni na TCB 3652 la tatu kutoka kichwa cha treni.

Mabehewa mengine yaliyopata ajali ni TCB 3650 la nne kutoka kichwa cha treni, 3619 la tano kutoka kichwa cha treni na la mwisho RCB 4526.

Aidha, taarifa hiyo iliyosainiwa na Mkuu wa kitengo cha mawasiliano cha TRC, Jamila Mbarouk ilidai uchunguzi wa chanzo cha ajali hiyo unaendelea kufanyika na shirika litaendelea kutoa taarifa juu ya tukio hilo.

Wakati huohuo, mapema leo asubuhi Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, alitembelea majeruhi wa ajali hiyo waliolazwa Hospitali ya mkoa wa Dodoma.

Akiwa hospitalini hapo aliushukuru uongozi wa mkoa wa Dodoma, Shirika la Reli Tanzania (TRC) pamoja na Wizara ya Afya na Mganga mkuu wa Serikali kwa ushirikiano walionyesha kuhakikisha majeruhi wote wanapata matibabu.

Alisema hadi majira ya saa saba jana Jumamosi usiku, walipata taarifa ya kuwa watu wote wameshaondolewa katika eneo la ajali ilipotokea.

Makamu wa Rais huyo alitembelea wodi nne na kuona majeruhi wanaendelea vizuri, huku wale waliovunjika mikono na miguu tayari wamefanyiwa upasuaji na kuendelea na matibabu menmgine hospitalini hapo.

Kadhalika Makamu wa Rais, alisema TRC kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa itasimamia kuhakikisha wagonjwa hao watakaporuhusiwa wanapatiwa usafiri wa kuelekea katika mikoa yao.

Mganga mkuu wa serikali, Prof. Habel Makubi, alisema wamepokea majeruhi 65, na wengine 25 walibakizwa hospitali ya Bahi kuendelea na matibabu, kutokana na hali zao kuwa vizuri.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Puma Energy Tz: Watanzania tudumishe amani kuvutia uwekezaji

Spread the loveKAMPUNI ya Mafuta ya Puma Tanzania imewakutanisha wadau mbalimbali katika...

Habari Mchanganyiko

DAWASA waanza utekelezaji agizo la Samia

Spread the loveMamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam...

Habari MchanganyikoKimataifa

Zuma akataliwa kugombea urais

Spread the loveTUME Huru ya Uchaguzi Afrika Kusini (IEC) imemwondoa rais wa...

KimataifaTangulizi

Zuma akataliwa kugombea urais

Spread the love  TUME Huru ya Uchaguzi Afrika Kusini (IEC) imemwondoa rais...

error: Content is protected !!