RAIS John Magufuli ameivunja Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchikavu na Majini (SUMATRA) ikiwa ni muendelezo wa hatua anazochukua kufuatia ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere, iliyopoteza mamia ya Watanzania. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Taarifa ya kuvunjwa kwa bodi ya wakurugenzi wa SUMATRA imetolewa leo tarehe 24 Septemba 2018 na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa, pia Rais Magufuli ametengua uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa SUMATRA, Mhandisi John Ndunguru.
“Mhe. Rais Magufuli amechukua hatua hiyo kufuatia ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere iliyotokea tarehe 20 Septemba 2018 na matukio mbalimbali ya ajali za barabarani hapa nchini yanayosababisha vifo, ulemavu na uharibifu wa mali,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa, Kamati ya Uchunguzi kuhusu ajali ya MV Nyerere inayotarajiwa kutangazwa hapo baadae na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa itaendelea na uchunguzi wa ajali hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kama ilivyopangwa.
Ajali ya MV Nyerere ilitokea tarehe 20 Septemba 2018 wakati kivuko hicho kikitokea Bugorora kisiwani Ukerewe kuelekea Kisiwa cha Ukara, ambapo watu takribani 224 wamepoteza maisha na majeruhi wakiwa 40.
Leave a comment