SERIKALI ya Tanzania, imeagiza uongozi wa shule, vyuo na taasisi za elimu zenye wanafunzi wengi, ziweke utaratibu wa kuingia kwa awamu ‘Shifting’, ili kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (Covid-19) . Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Jumapili, tarehe 4 Julai 2021 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi, akitoa muongozo mpya wa taasisi za elimu, wa udhibiti maambukizi ya Covid-19, jijini Dodoma.
“Kwa shule na vyuo vyenye wanafunzi wengi, Uongozi uweke utaratibu mzuri wa wanafunzi kuingia madarasani kwa awamu (shifting). Walezi wa mabweni (patron na matron) wapewe mafunzo na namna ya kubaini ishara na mabadiliko ya mwanafunzi, pia wafanye ukaguzi mara kwa mara wa mabweni na afya za wanafunzi,” amesema Pro. Makubi.
Pia, Prof. Makubi ameagiza wanafunzi wa vyuo, sekondari na shule za msingi, wavae barakoa kipindi chote wanapokuwa darasani na wanapokuwa katika vikundi vya majadiliano.
Sambamba na kuzingatia kukaa umbali wa mita moja, au zaidi na inapobidi wakati wa majadiliano wasizidi wanne.
Aidha, Prof. Makubi amesema matumizi ya Teknolojia, Habari na Mawasiliano (Tehama), yanaweza kutumika katika kufundishia kadri itakavyoelekezwa na taasisi husika ili kupunguza maambukizi.
Leave a comment