MBUNGE wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo (CCM), ameongoza harambee ya ujenzi wa shule mpya ya Sekondari ya Muhoji, inayojengwa ili kutatua changamoto ya mrundikano wa wanafunzi shuleni katika Kata ya Bugwema, mkoani Mara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara…(endelea).
Harambee hiyo ilifanyika jana tarehe 24 Januari 2023 na kuhudhuriwa na wananchi mbalimbali ambao wametoa michango yao.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge Jimbo la Musoma Vijijini, Prof. Muhongo amechangia saruji mifuko 150, wakati Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dk. Halfan Haule akichangia mifuko 20, huku wanakijiji wakiongozwa na Diwani wa Kata ya Bugwema, Clifford Machumu, wakichangia mifujo 124 na fedha taslimu Sh. 305,000.
“Michango hiyo ya wananchi ni mbali na michango Yao mingine ya nguvu kazi, kama kusomba mawe, mchanga na kokoto, pamoja na kutoa Sh. 45,000 kwa kila kaya,” imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imesema kuwa, malengo ujenzi wa shule hiyo itakayokuwa na vyumba vinne vya madarasa vyenye ofisi mbili mbili za walimu na choo chenye matundu nane, ukamilike kabla ya Julai 2023 ili ifunguliwe Januari 2024.
Ujenzi wa shule hiyo itasaidia kutatua changamoto ya mrundikano wa wanafunzi darasani pamoja na kutembea umbali mrefu, iliyotokana na kata hiyo kuwa na shule ya sekondari moja inayotumiwa na wanafunzi kutoka vijiji vinne.
Leave a comment