SERIKALI iko katika hatua za mwisho za maandalizi ya mfumo wa kielektroniki, wa kufuatilia usambazaji wa dawa katika hospitali, vituo vya afya na zahanati za umma, ili kudhibiti wizi wa dawa hizo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Alhamisi, tarehe 24 Juni 2021 na Naibu Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, David Silinde, akimjibu Mbunge wa Sumve (CCM), Kasalali Mageni, aliyehoji mpango wa Serikali katika kudhibiti wizi wa dawa, unaofanywa na baadhi ya watumishi wa umma wasiokuwa waaminifu.
“Sasa hivi Serikali tuko katika hatua ya mwisho za kuandaa mfumo ambao utakuwa uanjua dawa inayoingia na kutoka kiteknolojia. Naamini hii itakuwa suluhisho ya changamoto iliyopo sasa,” amesema Silinde.
Naibu Waziri huyo wa Tamisemi, amekiri uwepo wa changamoto ya wizi wa dawa, unaofanywa na baadhi ya watumishi wa umma wasiokuwa waaminifu.
“Katika moja ya changamoto ambayo imetukumba, Serikali imekuwa inapeleka dawa lakini haziwafikii walengwa kama ilivyokusudiwa. Sababu kubwa ilikuwa baadhi ya watumishi kutokuwa waaminifu,”amesema Silinde na kuongeza:
“Aidha kwa kuuza dawa au wengine kutozitumia mpaka zina kwisha muda wake wa matumizi, matokeo yake wale wagonjwa wanaoatakiwa kupata huduma ya msingi, wanashindwa kuzipata.”
Awali, Mageni alisema Serikali imeongeza fedha katika bajeti ya ununuzi wa dawa, kutoka Sh. 31 hadi 270 bilioni, lakini ongezeko hilo haliakisi idadi halisi ya dawa zinazopelekwa katika hospitali, vituo vya afya na zahanati za umma.
“Kwa kuwa bajeti ya dawa ya Serikali imeongezeka kama ambavyo taarifa zinaonesha, kutoka Sh. 31 mpaka 270 bilioni, na makabrasha ya Serikali yanaonesha upatikanaji wa dawa umeongezeka kwa kiasi kikubwa, lakini uhalisi kwenye vituo vya afya na zahanti, si sawa na hizi taarifa,” amesema Mageni na kuongeza:
“Wizara haioni imefika wakati muafaka kuweka utaratibu mahususi, ambao utaisaidia Serikali kwenda kutatua tatizo hilo kwa uhalisia kwa kupata taarifa halisi kwenye vituo na sio makrabasha yanayopatikana?”
Leave a comment