MWALIMU wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Dar es Dar es Salaam Ally Issa amebuni dawa ya asili ya ‘Lab Natural Pesticides’ (Muarobaini) kwa ajili ya kuwauwa wadudu waharibifu kwenye mazao.
Ally ambaye ni mtaalam wa maabara amesema amebuni dawa hiyo baada ya kuona adha wanayopitia wakulima nchini. Anaripoti Selemani Msuya, Mbeya … (endelea).
Ally ambaye ameshiriki Maonesho ya Nanenae yanafanyika katika Viwanja vya John Mwakangale mkoani Mbeya ameiambia Mwanahalisi Online kuwa dawa hiyo ya Lab Natural Pesticides inatokana na mti wa Muarobaini ambao umekuwa ukitumika kwa ajili ya matibabu ya magonjwa mengine.
“Moja ya changamoto ambayo mkulima anapitia ni kutumia dawa za madukani ambazo zina kemikali nyingi ambazo zinaathari kiafya, ila dawa hii ya asili haina madhara yoyote, hivyo amewataka wakulima kutumia dawa hiyo inayotengenezwa VETA,” amesema.
Amesema mti wa Muarobaini ni moja ya miti ambayo ni muhimu katika kupambana na wadudu waharibifu kwenye mazao na hauna kemikali zenye madhara kwa binadamu.
Mtaalam huyo amesema iwapo juhudi za kutumia malighafi asilia katika kutengeneza dawa za kupambana na wadudu vamizi kwenye mazao wakulima watakuwa salama na kilimo kitakuwa kwa kasi.
Aidha, amesema matumizi ya dawa ya muarobaini yatapunguza sumu kwenye mazao na kuongeza uzalishaji.
Mbunifu huyo amesema pia wametengeneza mbolea ambayo haina kemikali, ili wakulima kuachana na mbolea za viwandani ambazo zinaharibu uhalisia wa udongo.
“Wakulima wanapambana kutumia mbolea za madukani ambazo zina kemikali, ila sasa tumewaletea mbolea ambayo ni asili na mtu akitumia hakuna madhara ambayo anayapata na ardhi inakuwa salama,” amesema.
Mwalimu huyo amewataka wanasayansi kutumia taaluma zao kubuni dawa na mbolea asili ambazo zinafaa kutumika katika kilimo ili kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya mkulima.
Leave a comment