SAID Stephen na mtoto wake wa kike (jina linahifadhiwa), wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Morogoro kwa tuhuma za kuhusika kwenye mauaji ya mtoto Greyson Valentino, aliyekuwa na umri wa mwaka mmoja na miezi saba. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Wilbroad Mutafungwa, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro leo tarehe 24 Julai 2019 amesema, maiti ya mtoto huyo imekutwa shambani kwa Said.
Mtoto wa Said mwenye umri wa miaka minane, anayesoma Darasa la Pili katika Shule ya Msingi Mpapa iliyopo wilayani Mvomero, anatuhumiwa kuhusika na mauaji hayo.
Taarifa zaidi zinaeleza, tukio hilo lilitokea tarehe 21 Julai 2019 mchana katika Kijiji cha Hembeti, Mvomero mkoani humo.
Siku ya tukio, Kamanda Valentino ameeleza kuwa baba wa marehemu alikuwa kanisani, na kuwa alipata taarifa ya mwanaye kupotea ndipo aliporejea nyumbani na kuanza kumtafuta.
Katika harakati hizo, walipita shambani kwa Said na kuukuta mwili wa mwanaye ukiwa na majeraha kichwani.
Baba wa marehemu alikwenda nyumbani kwa Said kutaka kujua sababu za mwili huyo kukutwa shambani kwake, ndipo mtoto mwingine nyumbani hapo alipoeleza kuwa alimwona dada yake akimpiga kwa panga mtoto huyo na baadaye kumpeleka shambani.
Baada ya maelezo hayo, wananchi walimchukua mtoto huyo na panga lililotumika kwenye mauaji na kisha kumpeleka kwenye Kituo cha Polisi cha Dakawa.
Kamanda Mutafungwa amesema, hata baada ya baba wa mtoto huyo kupewa taarifa hizo na kuambiwa anatafutwa, hakujitokeza mpaka aliposakwa ndio akapatikana na kwamba, jeshi hilo linaendelea na uchunguzi zaidi. Tayari maiti ya mtoto huyo imekabidhiwa kwa wazazi wake.
Leave a comment