MTAMBO wenye uwezo wa kuzalisha Megawati 45 za umeme mali ya Kampuni ya uzalishaji na usambazaji umeme nchini – Aqua Power Tanzania Limited unatarajiwa kupigwa mnada baada ya wamiliki wake kushindwa kulipa deni katika Benki ya I&M Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Hatua hiyo imekuja baada ya kampuni ya Uwakili ya ADCA Veritas Law Group ambayo imeteuliwa na Benki hiyo kuwa msimamizi wa mali za Aqua Power Tanzania Limited kuanzia Oktoba mwaka huu, kutangaza zabuni kwa mtambo huo pamoja na mali nyingine za kampuni hiyo.
Kiwanda cha kampuni hiyo ambacho huzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia kinapatikana katika kijiji cha Hiari Kata ya Mayanga wilaya ya Mtwara Vijijini mkoani Mtwara vijijini.
Akizungumza na MwanaHalisi online, Mkurugenzi wa kampuni hiyo ya Uwakili – ADCA Veritas Law Group, Adronicus Byamungu alisema kampuni hiyo ya Aqua Power ilikuwa inanunua gesi asilia kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).
Alisema baada ya kuchakata gesi hiyo na kuzalisha umeme huo, ulikuwa unauzwa kwa kampuni ya Dangote inayojishughulisha na uzalishaji wa Saruji mkoani Mtwara.
Pamoja na mambo mengine, Byamungu alisema kampuni hiyo iliyoanzishwa mwaka 2017, mwaka huohuo ilikopa fedha kwa ajili ya uendeshaji wa kiwanda hicho lakini hadi sasa ilishindwa kulipa deni hilo katika benki ya I&M Tanzania.
Hata hivyo, alisita kutaja kiwango halisi cha deni hilo kwa mujibu wa sheria huku akisisitiza kuwa mzabuni atakayejitokeza atapewa fursa ya kutembelea kiwanda hicho na kutaja bei anayoitaka kulingana na soko la dunia.
Aidha, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa umma na kampuni hiyo ya uwakili kukaribisha wawekezaji kushindania zabuni hiyo, inaeleza kuwa kampuni hiyo ya Aqua Power Tananzania Ltd. hapo awali ilikuwa inafahamila kwa jina la Turbine Tech Ltd.
Hata hivyo, kwa mujibu wa nyaraka za Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni nchini (BRELA), inaonesha kuwa kampuni hiyo ya Aqua Power Tanzania Limited inamilikiwa na wanahisa watatu ambao ni Gachao Kiunq raia wa Uingereza kama Mkurugenzi Mkuu, Ekaterina Dyachenko raia wa Urusi kama Mkurugenzi mwenza na Bertha Alfaksaidi Lema raia wa Tanzania kama mkurugenzi mtendaji.
Taarifa hiyo ya Mawakili iliyotolewa kwa umma mwishoni mwa wiki inafafanua kuwa kampuni hiyo ya Aqua Power Tanzania iliweka dhamana ya mtambo huo, ofisi na mali nyingine kama magari kupata mkopo wa uendeshaji tarehe 7 Agosti 2017 ambao hata hivyo haujatajwa kiasi chake.
“Kwa mujibu wa maagizo mahususi niliyopewa na mwenye dhamana na kwa kutumia mamlaka yanayotokana na Hati fungani tajwa na tofauti zake pamoja na Sheria ya Makampuni Sura ya 212 R.E 2002 na Marekebisho yaliyofanywa hivyo; Nilichukua umiliki wa mali zote zilizotozwa chini ya Hati fungani iliyotajwa (“Mali Zinazotozwa”).
“Kwa sababu hiyo, kuanzia tarehe 26 Oktoba, 2022 natangaza mauzo ya mali za Kampuni hiyo zilizowekwa kama dhamana na nilizokabidhiwa… kwamba nakaribisha zabuni yake kwa ajili ya mauzo ya sehemu ya mali zinazotozwa kama ilivyobainishwa,” ilisema taarifa hiyo iliyotolewa kwa umma.
Aidha, taarifa hiyo ilitaja mali inayolipishwa au kuuzwa kuwa ni kiwanda cha kuzalisha umeme chenye majenereta matatu ya Gesi yenye uwezo wa kuzalisha Megawati 45 ambapo kila moja ina uwezo wa kuzalisha Megawati 15.
Mbali na mitambo hiyo, zabuni hiyo inajumuisha magari na ofisi za kiwanda hicho zilizojengwa kwenye eneo la mita za mraba 15,807 kwenye Kiwanja Na. 1 Kitalu A eneo la Hiyari, Wilaya ya Mtwara Vijijini.
Mali hiyo inajumuisha jengo la utawala na majengo mengine ya ziada kama vile karakana na vyoo.
“Kiwanda kinafikika kwa njia ya lami kando ya Barabara ya Nanyamba takriban kilomita 4 kutoka Barabara ya Mtwara-Dar es Salaam na takriban Kilomita 28 magharibi mwa Kituo cha Mji wa Mtwara. Alama za jirani ni pamoja na ofisi ya bomba la gesi la TPDC na kiwanda cha Saruji cha Dangote,” ilisema taarifa hiyo.
Kutokana na hali hiyo kampuni hiyo ya Uwakili imekaribisha wawekezaji wanaotaka kuwasilisha zabuni kuhusu mauzo ya kiwanda hicho kwamba bei ya ofa ya kiwanda kabla ya saa 10:00 Ijumaa siku ya Ijumaa tarehe 6 Januari, 2023.
“Baada ya hapo itafuatiwa na ufunguzi wa zabuni saa 10.00 jioni katika ofisi yangu ambapo wazabuni wanaalikwa kuhudhuria. Zabuni pia zinaweza kuwasilishwa kupitia barua pepe kwa adronicus@adcaveritaslaw.co.tz ili kupokelewa kabla ya tarehe ya mwisho,” imesema taarifa hiyo.
Kwa nini hawataki kutaja deni? Hapo kuna walakini. Hizo pesa ni za Watanzania walioweka katika benki hiyo