MBUNGE wa Geita Mjini, Joseph Kasheku ‘Msukuma’, ameibua vicheko bungeni, huku baadhi ya wabunge wakimtunza fedha, kufuatia hatua yake ya kumuuliza swali Mhandisi Habibu Mnyaa, ambaye ni mgombea ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), kwa kutumia lugha ya kingereza, swali kwa kutumia lugha ya kingereza. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Msukuma ambaye mara kadhaa amejinasibu bungeni kwamba ana elimu ya darasa la saba, aliibua vicheko hivyo leo Alhamisi, tarehe 22 Septemba 2022, bungeni jijini Dodoma, baada ya kukwama kumuuliza swali Mnyaa kwa lugha ya kingereza, kutokana na kutokujua kuzungumza lugha hiyo, hadi pale aliposaidiwa na mbunge aliye karibu yake.
Vicheko vilipamba moto bungeni hapo, mara baada ya Msukuma kusimama kuuliza swali, ambapo alianza kwa kuuliza “Thank you madame speaker for give me this chance, Mr. Mnyaa I want to ask you one question, where are you….” kisha akasita kitendo kilichofanya wabunge waendelee kucheka na kupiga meza.
Baada ya Msukuma kukwama kuendelea kuuliza swali kwa kingereza, mbunge mmoja aliyekuwa karibu yake alimtajia maneno ya kingereza akimtaka aulize, yaliyokuwa yanasema “What didi you do for the past five years.”
Baada ya Msukuma kutajiwa maneno hayo, aliendelea kuuliza swali akisema “What did you do for the last five years.”
Swali la Msukuma lilimaanisha “ulifanya nini katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.”
Baada ya Msukuma kuuliza swali hilo, Spika wa Bunge, Dk. Tulia Akson, alimuuliza Mnyaa kama amelielewa swali hilo, ambapo alijibu kuwa hajalielewa swali, kitendo kilichopeleka Spika Tulia kulirejea swali kwa kutumia Kingereza.
Mnyaa alijibu swali la Msukuma akisema, katika kipindi cha miaka mitano alichokuwa Mbunge wa EALA, alifanya mambo mbalimbali, ikiwemo kupitisha miswada mbalimbali ya sheria pamoja na kukwamisha muswada binafsi uliwasilishwa na mjumbe wa Kenya, ambao ulikuwa na lengo la kuharibu maslahi ya Tanzania.
“Katika kipindi cha miaka mitano tumepitisha miswada mingi, tumefanya vitu vingi vingine vilikuwa vinategema na kundi. Kulikuwa na muswada mmoja kutoka kwa mmoja wa wajumbe wa Kenya, ulikuwa muswada binafsi ambapo tuliweza kuusimamisha kwa sababu ulikuwa mbaya kwa uchumi wa nchi yetu, ungeharibu tamaduni zetu. Hicho ndicho moja ya kitu ambacho tulikikataa pamoja,” amejibu Mnyaa.
Awali akiomba kura kwa wabunge, Mnyaa aliomba achaguliwe akisema yeye ni mzoezi ndani ya bunge hilo ambao atautumia kutetea maslahi ya nchi.
Leave a comment