SHINDANO la Bongo Star Search (BSS) msimu wa 12 umezinduliwa huku jaji maarufu Salama Jabir akirejea ulingoni. Anaripoti Matilda Buguye (endelea).
Salama ambaye alikosekana katika mashindano hayo kwa misimu miwili mfululizo, sasa anarejea kuungana na majaji wenzake walioasisi shindano hilo takribani kumi iliyopita.
BSS msimu wa 12 umezinduliwa usiku wa kuamkia leo Alhamisi, tarehe 9 Septemba 2021, jijini Dar es Saaam ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Jokate Mwegelo.
Majaji wengine wa shindano hilo ambalo msimu huu litaanzia jijini Arusha tarehe 25 Septemba 2021, ni Ommy Dimpoz, Master J pamoja na Rita Polsen ‘Madam Rita’ ambaye ndiye jaji mkuu.
Akizungumza kwenye uzinduzi huo, Jokate alisema vijana wanapaswa kuamini katika muda, kukubali kujifunza kuheshimu na kushukuru kwa kila nafasi wanazozipata kutoka kwa watu.
Aliwataka wasipende kujiona wastahili na wenye majivuno ikiwa bado wanasafari ya kuyafikia mafanikio.
“Vijana wa siku hizi kidogo wanapenda vitu fasta, kijana ni lazima upitie kipindi fulani cha kuokwa, sisi hapa leo tupo hivi lakini tuna miaka kama kumi hivi ya kutengenezwa ili kufikia hapa tulipo,” alisema Jokate.
Leave a comment