MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini Tanzania, Jaji Francis Mutungi ameteua kikosi kazi cha watu 23 kinachojumuisha makundi mbalimbali ya wanasiasa, wanazuoni, asasi za kiraia na wanasheria ili kupitia hoja mbalimbali zilizotolewa na wadau wa demokrasia. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kikosi kazi hicho, kitakuwa chini ya Mwenyekiti, Profesa Rwekaza Mukandara, kitazinduliwa rasmi na kuanza kazi, tarehe 10 Januari 2022.
Kimeundwa baada ya kufanyika kwa kikao cha siku tatu kilichowakutanisha wadau mbalimbali wa demokrasia wa vyama vingi vya siasa kuanzia tarehe 15-17 Desemba 2021, jijini Dodoma wakiwemo viongozi waandamizi wastaafu.
Lengo la kikao hicho kilichofunguliwa na Rais Samia SuluhuHassan na kufungwa na Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi ilikuwa kuangazia hali ya demokrasia nchini na jinsi ya kutatua changamoto zinavyovikumba vyama vya siasa hususan vya upinzani kuzuiwa kufanya mikutano ya hadhara.
Hata hivyo, chama kikuu cha upinzani nchini cha Chadema na NCCR-Mageuzi havikushiriki kikao hicho kwa sababu mbalimbali.
Kikao hicho, kilimpa kazi Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kuandaa kikosi kazi kitakachokwenda kupitia hoja hizo na kuandaa mapendekezo yatakayowasilishwa kwa Baraza la Vyama vya Siasa.
Mara baada ya kuwasilishwa kwa baraza hilo linaloundwa na vyama vyote vya siasa vyenye usajili, litayapitia kisha kuyawasilisha serikalini kwa ajili ya utekelezaji.
Kikosi kazi hicho, kimetangazwa leo Alhamisi, tarehe 23 Desemba 2021 na Jaji Mutungi.
Soma taarifa yote na wajumbe hao hapa;
Leave a comment