MSAJILI wa Vyama Siasa nchini Tanzania, Jaji Francis Mutungi, amesema kikao chake na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) Simon Sirro, kimemsaidia kujua jeshi hilo lina nia njema na wanasiasa. Anaripoti Mwamdishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Jaji Mutungi ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, tarehe 23 Septemba 2021, baada ya kufanya mazungumzo na IGP Sirro jijini Dodoma, ikiwa ni maandalizi ya mkutano wa wadau wa vyama vya siasa nchini, unaotarajiwa kufanyika tarehe 21 Oktoba 2021.
“Mantiki ya vikao hivi tunataka tujaribu kupunguza misuguano ambayo wakati mwingine haina ulazima na leo kwa mara ya kwanza nimegundua, kumbe wakati mwingine Polisi wanakuwa na nia njema.”
“Kuna mambo tunayokuwa hatuyajui raia, lakini laiti wangekuwa kila kitu wanakieleza tungeanza mushuku kama tunafanya siasa au tunaleta fujo,” amesema Jaji Mutungi.
Jaji Mutungi amesema masuala yaliyoibuliwa katika kikao chake na IGP Sirro, atayafikisha katika mkutano wake na viongozi wa vyama vya siasa, unaotarajiwakufanyika tarehe 30 Septemba 2021, jijini Dar es Salaam.
Amewataka viongozi wa vya siasa nchini, kuutumia mkutano huo kutoa maoni yao kuhusu changamoto wanazokabiliana nazo, ili zifanyiwe kazi.
“Tutakapokaa kikao cha wadau nadhani tutakuwa na muelekeo mzuri, lengo langu kukusanya mambo kadhaa ambayo tutakuja tuyaunganishe kwenye vikao pengine tutakuja na mustakabali nzuri,” amesema
“Nimegundua polisi wametaja baadhi ya mapungufu wanayoona yapo kwenye sheria na sisi tukawakumbusha kwamba, kipindi hiki tuko kwenye kukusanya maoni mbalimbali ya marekebisho ya sheria ni vizuri watakapoombwa kuleta wasisahau kuyaleta,” amesema Jaji Mutungi
Amesema “Natarajia pia wanasiasa watatoa yale kama yaliyotolewa na Polisi, kweli tutafika mahali nchi tunakwenda tunakotakiwa.”
Naye IGP Sirro, amesema Jeshi la Polisi litaendelea kuwa karibu na viongozi wa vyama vya siasa kwa sabau ni wadau muhimu katika masuala ya ulinzi na usalama.
“Kimsingi tumekubaliana mengi ya kufanya kuhakikisha mwisho wa siku nchi yetu inakuwa ya amani na utulivu na niwaombe kwa sababu wanaendelea na forum ya kukutana na wanasiasa,” amesema IGP Sirro na kuongeza:
“Basi watakapokuwa wamekubaliana ni vizuri na sisi tukapata taarifa kwa sababu, lengo kuitumia taarifa na mwisho wa siku kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa ya amani na utulivu.”
Leave a comment