KAMANDA wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Camillius Wambura, amesema ameanzisha operesheni maalum ya kupambana na wahalifu wanaotumia silaha, maarufu kama majambazi. Anaripoti Jemima Samweli, DMC…(endelea).
Kamanda Wambura ametoa kauli hiyo leo Jumanne tarehe 25 Mei 2021, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam, baada ya kushiriki kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dar es Salaam.
Kauli hiyo ya Kamanda Wambura, imekuja siku nane baada ya tarehe 17 Mei 2021, kuteuliwa na Inspekta Jenerali wa Polisi nchini (IGP), Simon Sirro, kuchukua mikoba ya SACP Lazaro Mambosasa, kwenye kanda hiyo.
Mrithi huyo wa Kamanda Mambosasa amesema, ameanzisha operesheni hiyo baada ya kuibuka kwa matukio mawili ya ujambazi, yaliyotokea hivi karibuni maeneo ya Mbezi na Mabibo.
“Kufuatia matukio hayo, Jeshi limejikita katika operesheni mahsusi kupambana na wahalifu hawa, ili kurudisha hali ya usalama na amani katika Jiji la Dar es Salaam na kuruhusu wananchi wetu kuendelea na shughuli zao, bila woga wowote,” amesema Kamanda Wambura.
Kamanda Wambura amewaonya wahalifu hao akisema kwamba, hawana pa kukimbilia, huku akitoa mfano wa namna Jeshi hilo lilivyofanikiwa kuipata pikipiki iliyokamatwa Dar es Salaam, na kufichwa Gairo, mkoani Morogoro.
“Pamoja na pikipiki moja iliyoporwa Dar es Salaam tarehe 21 Mei 2021na kukimbizwa Gairo, tuliifuata kesho yake. Tunasema ukiiba Dar es Salaam hauko salama, hata kwenda nje ya Tanzania, hauko salama. kukimbia haikusaidii,” amesema Kamanda Wambura.
Kamanda Wambura ametuma salamu kwa wahalifu wote mkoani humo, akiwataka wasijaribu kupima kina cha jeshi hilo.
“Kwa watuhumiwa wote ambao wanadhani wanaweza kuitikisa Serikali, haijawahi kutokea mhalifu akashindana na Serikali na akashinda. Kitu pekee tunachoweza kuwaambia wakae chonjo, sasa ni wakati mbaya,” amesema Kamanda Wambura na kuongeza:
“Na kitu kingine tunachoweza kuwaambia, wasijaribu kupima kina cha maji, miguu yao ni mifuipi sana hawawezi kupima kina cha maji. Hawa watu wameshaelekezwa wasalimishe silaha, kumiliki silaha kinyume na sheria ni kosa la jinai, ili tupate silaha hiyo kutoka kwako, madhara yake ni makubwa sana.”
Leave a comment