WANANCHI wa Jimbo la Konde, Visiwani Zanzibar, leo Jumapili tarehe 18 Julai 2021, wanachagua mbunge wao, ili kuziba nafasi iliyoachwa wazi na Khatib Said Haji, aliyefariki dunia tarehe 20 Mei mwaka huu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Haji aliyekuwa Mbunge wa Konde kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, alifariki dunia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, jijini Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu. Mwili wake ulizikwa siku hiyo hiyo nyumbani kwao Pemba, Zanzibar.
Kufuatia kifo hicho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iliitisha uchaguzi huo mdogo, ambapo vyama 12 vimejitosa kulisaka jimbo hilo.
Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo,vinachuana vikali kulitwaa jimbo hilo.
ACT-Wazalendo kimemteua Mohammed Said Issa, kulitetea jimbo hilo lililokuwa linashikiliwa na mwanachama wake Khatib, aliyefariki dunia. Huku CCM kikimteua Sheha Mpemba Faki, kugombea jimbo hilo.
Khatib aliliongoza Jimbo la Konde kwa muda wa miaka 10 mfululizo, kupitia Chama cha Wananchi (CUF).Kuanzia 2010 hadi 2020.
2020 alihamia ACT-Wazalendo na kugombea jimbo hilo. Aliliongoza jimbo hilo kupitia chama hicho kwa muda wa miezi mitano, kuanzia tarehe 15 Disemba 2020, alipoapishwa kuwa Mbunge na Spika Job Ndugai, hadi alipofariki dunia Mei 2021.
Leave a comment