MKURUGENZI wa Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam, Beatrice Dominic amemkabidhi Ramadhan Kwangaya, ofisi ya Meya wa Manispaa hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hafla hiyo fupi imefanyika leo Jumatatu tarehe 12 Mei 2020 katika ofisi hizo na kuhudhuriwa na madiwani na wakuu wa idara na vitengo.
Kwangaya ambaye ni naibu meya na diwani wa Manzese kupitia Chama cha Wananchi (CUF) anakaimu nafasi ya meya baada ya Boniface Jocob kupoteza sifa za kushirikia nafasi hiyo.
Taarifa iliyotolewa na kitengo cha habari na uhusiano, imesema Mkurugenzi wa manispaa hiyo, Beatrice amemkabidhi Kwangaya gari kwa ajili ya matumizi ya shughuli zake za kiofisi.
Pia, amekabidhiwa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/20 pamoja na kanuni za Halmashauri kama nyenzo zitakazomsaidia kutekeleza majukumu yake ya kila siku.
Jacob alipoteza nafasi ya umeya baada ya barua inayoelezwa kuandikwa tarehe 28 Aprili 2020 na katibu wa Chadema Kata ya Ubungo kwenda kwa mkurugenzi wa halmashauri kuonyesha amevuliwa uanachama hivyo kupoteza sifa za kuwa meya.
Hata hivyo, Jacob mwenyewe, Chadema makao makuu na mtu huyo ambaye jina lake lilitumika kwenye barua hiyo kudai haina ukweli, kwani hakuna kikao chochote kilichokaa cha kumjadili Jacob kisha kumvua uanachama.
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) ilisema kama Jacob anaona kuna kasoro, anapaswa kuchukua hatua mbili. Mosi, aende mahakamani au akate rufaa kwa kuandika barua kwa waziri wa Tamisemi ambaye atalishughurikia.
Leave a comment