AUGUSTINO Mrema, Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha TLP, amemtaka Rais John Magufuli kuwa macho anapofanya uteuzi wa viongozi wa umma, huku akimshauri kufuata nyayo za Rais Mstaafu wa Awamu ya tatu, Benjamin Mkapa. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Mrema ametoa ushauri huo leo terehe 27 Julai, 2018 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na wanahabari kuhusu masuala mbalimbali yanayoendelea nchini, ambapo amesema Rais Mkapa wakati wa utawala wake alikuwa anateua watu wenye sifa stahiki.
Mrema amesema kitendo ambacho amekiita kuwa ni cha ‘kuokoteza okoteza’ kimepelekea baadhi ya watu kwenye wizara mbalimbali kufanya mambo ya ajabu ambayo Rais Magufuli hayajui.
“Rais awe macho sana, hawa watu wa kuokoteza okoteza hawafai, ujifunze kwa Rais Mkapa,” amesema Mrema.
Katika hatua nyingine, Mrema amesema amependezwa na utendaji kazi wa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola ambapo amesema yuko tayari kumuonyesha njia alizopitia katika kuiongoza wizara hiyo miaka kadhaa iliyopita wakati akiwa Waziri.
“Lugola amenipendeza kwa kile kitendo cha kufuatilia mbwa wa polisi, si jambo dogo sababu watu wengi wanajiuliza inakuaje mbwa wa polisi anatumika kulinda majumba ya watu,” amesema.
Leave a comment