MAHAKAMA Kuu, Kanda ya Kusini imemuachia huru kwa dhamana, Seleman Mathew, aliyekuwa mgombea Ubunge wa Jimbo la Mtama mkoani Lindi ambaye pia ni mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) katika mkoa huo, anaandika Mwandishi Wetu.
Tarehe 8 Februari, mwaka huu Mathew pamoja na Ismail Kupulila, katibu wa Chadema kata ya Nyangamala walihukumiwa kifungo cha miezi nane jela katika Mahakama ya Mkoa wa Lindi kwa kosa la kufanya mkutano wa hadhara bila kibali.
Wakili wa washtakiwa Deusdedit Kamalamo amesema, “unapokuwa umefungwa unaweza kuishawishi mahakama kuwa nje kwa dhamana wakati ukisubiri rufaa ndiyo maana tukifungua madai kwa hati ya dharura na Jaji amekubaliana na hoja zetu.”
Kesi namba 1 ya mwaka 2017 katika Mahakama ya Rufaa ambayo Mathew na mwenzake wamefungua kupinga kuhukumiwa kifugo cha miezi nane jela inatarajiwa kusikilizwa tena tarehe 3 Mei mwaka huu.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 Mathew aligombea ubunge katika Jimbo la Mtama, Lindi Vijijini kupitia Chadema ambapo ndiye aliyekuwa mpinzani mkuu wa Nape Nnauye, Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo.
Mathew pia ameendelea kujiimarisha katika jimbo hilo kupitia vikao vya ndani kuelekea uchaguzi wa 2020.
Leave a comment