MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC) nchini Tanzania, Amos Makalla amesema, tarehe 6 Novemba 2021, atazindua mpango wa kulifanya Jiji hilo kuwa safi na lenye kuvutia kibiashara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Aidha amesema, shughuli ya kuwaondoa wafanyabiashara maeneo yasiyoruhusiwa kama kwenye njia za watembea kwa miguu, waliojenga juu ya mitaro na mifereji litamalizika tarehe 30 Oktoba 2021.
RC Makalla amesema hayo leo Jumatano, tarehe 20 Oktoba 2021, wakati akizungumza na waandishi wa habari, kuelezea hali inavyoendelea ya kuwapanga kwenye maeneo sahihi ya kufanyia biashara.
“Yaani ikifika tarehe 30 Oktoba, nikitoka hapa ofisini (zilizopo Ilala) hadi Kibaha au hadi Bagamoyo nisione kibanda chochote barabarani. NI wakati wa wafanyabiashara kuhama wenyewe kwa hiyari yenu,” amesema
“Nataka kuona mitaro na mifereji yote ikiwa safi. Wakati mwingine vibanda hivyo vilikuwa vinasababisha uchafu, mtu anachinja kuku au anamwaga maji machafu,” amesema Makalla.
Akisisitiza hilo, RC Makalla amesema “ni matarajio yangu, njia zote Dar es Salaam za watembea kwa miguu zitakuwa wazi. Kariakoo inapitika wakati wote na tukifanya hivyo tutaifanya Dar es Salaam kuwa safi na tarehe 6 Novemba, nitazindua mpango wa kuifanya Dar es Salaam kuwa safi.”
“Kuifanya Dar es Salaam ipendeze, kuna mambo yatakuwa surprise na matarajio yangu, Dar es Salaam itaendelea kuwa kitovu cha biashara katika mazingira safi. Serikali inakwenda kutengeneza mazingira mazuri,” amesema
Makalla amesema, katika kitabu hicho, ataeleza mikakati mbalimbali na kuwataka wananchi kukaa mkao wa kula kuusubiri.
Mkuu huyo wa mkoa, ametoa pongeza kwa makundi mbalimbali ikiwemo waandishi wa habari kwa kuunga mkono shughuli hiyo kwa ufanisi na kuwaomba kuendelea pasina kuchoka kwani jamii inawategemea.
Leave a comment